SIMBA WAONESHA UBISHI

Simba wameonyesha kuwa wao ni wabishi kwenye soka kwa sasa baada ya jana kufanikiwa kuwachapa Mlandege bao 1-0 kwenye mchezo wa Kombe la Mapinduzi Kundi A, uliopigwa kwenye Dimba la Amaan.

Simba wamefanikiwa kushinda michezo yao yote ya kundi na hivyo wamemaliza kwa kukusanya pointi tisa kwenye kundi hilo.

Katika mchezo wa jana, Haruna Niyonzima ndiye alikuwa shujaa wa Simba baada ya kuifungia timu hiyo bao pekee kwa mkwaju wa penalti katika dakika ya 20 ya mchezo

Niyonzima alifunga bao hilo baada ya beki wa timu hiyo, Asante Kwasi kuangushwa kwenye eneo la hatari na mwamuzi kuamuru mkwaju wa penalti.

Hata hivyo, kipindi cha pili Mlandege walionekana kuwika zaidi kwenye eneo la kiungo lakini walishindwa kuipenya ngome ya Simba ambayo ilikuwa inaongozwa na Kwasi, Poul Bukaba na Hassan Mlipili ambao walionyesha kiwango cha hali ya juu.

Mbali na Simba timu nyingine ambayo imefuzu kwenda nusu fainali ni KMKM, huku Kundi B, Azam na Malindi nazo zikienda hatua hiyo.

Lakini kuna uwezekano mkubwa Simba ikakutana na kigingi kwenye hatua inayofuata kwa kuwa baada ya mchezo wa jana watabadilisha kikosi na wachezaji wengi wa kikosi cha kwanza watarejea Dar es Salaam kucheza mchezo wa hatua ya Makundi wa Klabu Bingwa Afrika dhidi ya JS Saoura kwenye Uwanja wa Taifa.

Moja ya timu ambayo Simba wanaomba wasipangwe nayo ni Azam ambayo iliwachapa wapinzani wao Yanga mabao 3-0 kwenye mchezo wa Kundi B.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527