KOCHA SIMBA ATEMA BEKI NA MSHAMBULIAJI


Kocha Patrick Aussems

Kocha Mkuu wa klabu ya Simba, Patrick Aussems amesema hajawajumuisha wachezaji wake wawili katika kikosi cha wachezaji 23 wanaojiandaa na michuano ya SportPesa.

Aussems amesema kuwa amemwacha mchezaji Yusuph Mlipili pamoja na Adam Salamba ili kuwapa nafasi wachezaji wawili waliokuja kwaajili ya majaribio, ambao atawatumia katika michuano hiyo ya SportPesa.

"Nilichokisema toka mwanzo ni kuwa katika michuano ya SportPesa tutaruhusu wachezaji watatu au wanne kwaajili ya majaribio na wapo hivi sasa katika kikosi chetu cha wachezaji 23", amesema Aussems.

"Katika kundi letu la wachezaji 23, tumewaacha wachezaji, Yusuph Mlipili pamoja na Adam Salamba", ameongeza kocha huyo.

Pia kocha huyo amesema kuwa timu yake inakabiliwa na michezo mingi hivi sasa na hakuna namna zaidi ya kupambana na kushinda, ambapo itacheza mchezo mmoja kila baada ya siku tatu.

"Tuna michezo 14 inatukabili, na baadhi ya klabu katika ligi zimeshacheza michezo 22 kwahiyo inamaanisha ni tofauti ya michezo 8, inaogopesha na inabidi TFF ifanye utaratibu wa kurekebisha ratiba yetu, utaratibu ufanyike tucheze mchezo mmoja kila baada ya siku tatu".

Simba inatarajia kushuka dimbani jioni ya leo katika mchezo wake wa kwanza wa michuano ya SportPesa, ambapo itavaana na AFC Leopards ya Kenya . Imesema kuwa itawatumia wachezaji wawili walio katika majaribio, ambao ni Lamine Moro kutoka Ghana (beki) na Hunlede Kissimbo Ayi-Abel kutoka Togo (mshambuliaji) na wakifanya vizuri watasajiliwa kwa ajili ya michuano ya kimataifa na Ligi Kuu Tanzania Bara.

Via EATV

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527