AZAM FC NA SIMBA FEBRUARI 22 NA YANGA APRILI 29 UWANJA WA TAIFA

Bodi ya Ligi Kuu Tanzania Bara (TPLB) imepanga ratiba za mechi za viporo za Klabu Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati, Azam FC, itakazocheza dhidi ya Simba na Yanga zilizotakiwa kufanyikwa kwenye raundi ya kwanza.

Ratiba hiyo mpya inaonyesha kuwa Azam FC itacheza mechi ya kwanza ya ligi dhidi ya Simba msimu huu, Februari 22 mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam huku ile na Yanga ikipigwa Aprili 29 mwaka huu.

Mechi nyingine mbili za viporo za Azam FC, dhidi ya Mbeya City na Ndanda, ilizotakiwa kucheza kwenye raundi mbili za awali za mzunguko wa pili wa ligi hiyo, itakipiga na City Aprili 14 mwaka huu kwenye Uwanja wa Sokoine, kabla ya kusafiri hadi mkoani Mtwara kumenyana na Ndanda Aprili 18.

Katika mabadiliko hayo ya ratiba inaonyesha kuwa, msimu wa ligi utafungwa Mei 26 mwaka huu kwa mechi zote kupigwa huku Azam FC ikitarajiwa kufunga pazia hilo kwa kumenyana na Yanga, mchezo utakaopigwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Wiki hii Azam FC inatarajia kukamilisha raundi ya 24 ya ligi kwa kucheza na Biashara United, mchezo utakaofanyika Uwanja wa Azam Complex Ijumaa hii saa 1.00 usiku, kabla ya kuhamishia nguvu kwenye Kombe la Shirikisho (Azam Sports Federation Cup) ikitarajia kukipiga na Pamba kwenye dimba hilo Januari 28 mwaka huu saa 1.00 usiku.

Azam FC hadi sasa imeonekana kufanya vizuri kwenye msimu huu wa ligi, ikiwa ni miongoni mwa timu zinazopigana vikumbo kuwania taji hadi sasa ikiwa nafasi ya pili ikiwa imejikusanyia pointi 44 ikizidiwa pointi tisa na Yanga iliyo kileleni, lakini matajiri hao wakiwa na mchezo mmoja mkononi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527