NDEFU ZAIDI DUNIANI ‘AIRLANDER 10’ NDEGE YAPATA KIBALI CHA KUANZA MATENGENEZO

Sampuli ya awali ya Airlander iikiwa katika majaribio

Ndege ndefu zaidi duniani ipo tayari kwa ajili ya kuanza kutengenezwa kibiashara na kupakia abiria.

Hatua hiyo inakuja baada ya sampuli ya awali ya Airlander 10 yenye thamani ya pauni milioni 32 - ambayo ni mjumuiko wa ndege na meli inayopaa - kustaafishwa rasmi baada ya kufaulu majaribio ya mwisho.

Kutokana na mafanikio hayo, kampuni iliyobuni ndege hiyo ya Hybrid Air Vehicles (HAV) yenye maskani yake Bedford, Uingereza imepewa ruhusa na mamlaka ya usafiri wa anga wa kiraia wa nchi hiyo Civil Aviation Authority (CAA) kuanza uzalishaji wa aina hiyo ya ndege.

Kampuni hiyo awali mwezi wa Oktoba 2018 ilipewa kibali cha usanifu kutoka kwa mamlaka ya usalama wa usafiri wa kiraia barani Ulaya European Aviation Safety Agency (Easa).
Airlander 10 baada ya kuanguka Novemba 18, 2017 wakati wa safari ya majaribio

Stephen McGlennan, ambaye ni mtendaji mkuu wa kampuni ya HAV amesema mwaka 2018 ulikuwa mzuri sana na kusema kibali cha Easa kilikuwa ni ishara kubwa.

Amesema kwa sasa azma ya kampuni yake ni kutengeneza ndege aina ya Airlander 10 kwa ajili ya biashara na kupakia abiria.

"Sampuli ya awali imetimiza kazi yake kwa kutusaidia kupata takwimu na taarifa muhimu tulizokuwa tukizihitaji ili kuvuka kutoka hatua ya sampuli mpaka utengenezwaji wa ndege halisi," amesema.

Kwa sasa matarajio ni kwamba ndege ya kibiashara itakamata mawingu ikiwa na abiria waliolipia safari yao miaka ya mwanzoni ya 2020.

HAV ilitenga kitita cha pauni milioni 32 baada ya sampuli ya awali kudondoka, na kuwaarifu wanahisa wake kuwa hiko ndicho "kiwango cha juu zaidi cha bima".

Vibali kutoka kwa CAA na Easa sasa vinaipa kampuni hiyo "nafasi imara ya kuanza uzaishaji".

HAV ilifanya majaribio ya awali ya Airlander 10 kutoka katika eneo lake la awali la uwanja wa ndege wa Cardington mwezi Agosti 2016 lakini walihama eneo hilo Juni mwaka jana.

Mwezi Julai wakatangaza mipango yao ya kutoa "huduma za kifahari" pale ambapo majaribio yote yatakapomalizika kwa mafanikio.
Chanzo - BBC

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527