RAIS MAGUFULI ASIKIA KILIO CHA SHEIKH MSIKITI WA UDOM

Rais John Magufuli amesikia kilio kilichofikishwa na Sheikh Mussa Kundecha, kuhusu kitendo kilichofanywa na uongozi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) cha kuvunja msikiti uliokuwa ukijengwa.

Amesema, kuwa suala hilo litashughulikiwa na kwamba, ni utaratibu wa kawaida kwa vyuo kuwepo kwa huduma ya nyumba za ibada kama ilivyo kwa Vyuo Vikuu vingine.

Sheikh Kundecha, Amiri Mkuu wa Baraza Kuu la Jumuiya na Taasisi za Kiislam asubuhi ya leo alimweleza Rais Magufuli kadhia iliyotokea UDOM na kumwomba kuliangalia suala hilo kutokana na umuhimu wake.

“Ni utaratibu wa kawaida, pale Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kuna Msikiti, madhehebu yote yanafanya ibada pale. Kuna Kanisa ambapo madhehebu yote yanafanya ibada pale, wanapangiana muda tu. Niseme hili la Dodoma litafanyiwa kazi,” amesema Rais Magufuli na kuongeza;

“Spiriti ile ile iliyokuwepo UDSM ndio itakayokuwepo Dodoma. Sisi Tanzania tumelelewa na Mwalimu Nyerere namna ya kuvumiliana. Uvumilivu huu tukiendelea kuujenga, utalifikisha taifa hili mahali pema.”

Awali Sheikh Kundecha alisema,
“Wiki moja iliyopita tulijiwa na wenzetu Waislamu kutoka Dodoma, wakiongelea suala la msikiti. Tunashukuru serikali kwa kutenga eneo la ibada, ni jambo muhimu,” amesema Sheikh Kundecha.

Amesema kuwa, ni muhimu kuwa na maeneo ya ibada katika maeneo ya kijamii hasa kutokana na utaratibu wa Ibada ya Kiislam na kwamba, kwa kuzingatia hilo uongozi wa chuo awali ulitoa eneo na Waislam walianza kuchangishana kwa ajili ya ujenzi wa msikiti huo.

“Waislam wakawa wanachangishana ili kujenga nyumba hiyo ya ibada lakini ghafla taarifa ya chuo ikatolewa kusitisha ujenzi wa msikiti huo,” amesema Sheikh Kundecha na kuongeza;

“Tuliamini labda taarifa hiyo ya kusitisha ilitolewa ili kuweka baadhi ya mambo sawa lakni mara wakaleta magreda na kuanza kuubomoa na na mnajua pesa za kuchangisha zilivyo ngumu. Sasa leo anasikia greda imevunja, hii inaleta shida kwa wanaochangia. Nakuomba maeneo ya namna hiyo uyatazame ili isilete mizozo.”

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527