MGONJWA MAHUTUTI KWA MIAKA 10 AJIFUNGUA MTOTO....HAJULIKANI ALIYEMPA MIMBA HOSPITALINI

Maafisa wa polisi mjini Arizona nchini Marekani wameanzisha uchunguzi wa unyanyasaji wa kingono baada ya kupokea ripoti kuhusu mgonjwa aliyekuwa katika koma kwa muongo mmoja kujifungua.



Mwanamke huyo ni mgonjwa katika kliniki moja inayosimamiwa na shirika la afya la Hacienda , karibu na mji wa Phoenix.

Klinki hiyo ya Hacienda haijatoa maelezo kuhusu tukio hilo lakini ikasema kuwa inaelewa kisa hicho.

Chombo kimoja cha habari kiliripoti kwamba mtoto aliyezaliwa yuko katika afya nzuri na kunukuu vyanzo vikisema kuwa wafanyikazi wa kliniki hiyo hawakujua kwamba mwanamke huyo alikuwa mjamzito.

Mgonjwa huyo bado hajatambulika.

Msemaji wa kituo cha polisi cha Phoenix alisema kuwa kuwa kisa hicho kwa sasa kinafanyiwa uchunguzi, lakini hakusema ni lini uchunguzi huo ulianzishwa ama hata kutoa maelezo ya kesi hiyo.

Mwanamke huyo iliripotiwa kwamba amejifungua mnamo mwezi Disemba 29. Kulingana na duru ambayo haikutajwa: hakuna aliyejua kwamba mwanamke huyo alikuwa mjamzito hadi alipoanza kuonyesha dalili za kutaka kujifungua.

Duru hizo pia zilisema kuwa mwanamke huyo alihitaji kuangaliwa kwa saa 24 na kwamba watu wengi wamekuwa wakiingia na kutoka katika chumba chake.

Mikakati ya kiusalama.

Itifaki katika hospitali hiyo imebadilika kilisema chanzo kingine na sasa wanaume wanaoingia katika vyumba vilivyo na wanawake ni sharti waandamane na wafanyakazi wanawake.

Katika taarifa, kliniki ya Hacienda ilisema '' hivi majuzi tuliarifiwa kuhusu kisa kibaya kinachohusisha afya na usalama wa ndani.

Imesema kuwa inashirikiana vizuri na maafisa wa polisi. David Leibowitz, ambaye ni msemaji wa Hacienda, aliongezea kwamba shirika hilo lilikuwa likitumia kila njia kubaini ukweli.

Idara ya afya katika jimbo la Arizona imesema kuwa imetuma wakaguzi kuwachunguza wagonjwa katika hospitali hiyo kwa lengo la kuweka sheria kali za kiusalama.

Katika tovuti yake, Kliniki ya Hacienda inasema kuwa inawaangalia vizuri wagonjwa wenye magonjwa sugu, wagonjwa vijana , watoto wachanga pamoja na wale walio na ulemavu.
Chanzo - BBC

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post