RAIS MAGUFULI AWATAKA WAISLAMU KUDUMISHA AMANI YA NCHI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli tarehe 17 Desemba, 2018 ameungana na Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) kuadhimisha miaka 50 ya tangu kuanzishwa kwa Baraza hilo.


Maadhimisho hayo yamefanyika katika ukumbi wa Diamond Jubilee Jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa, Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, Waheshimiwa Mabalozi wa Iran na Misri, viongozi wa vyombo vya ulinzi na usalama, viongozi wa Mkoa wa Dar es Salaam wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa huo Mhe. Paul Makonda, Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja Mhe. Vuai Mwinyi Mohamed, Wajumbe wa Baraza la Ulamaa na Masheikh wa Mikoa na Wilaya zote 26 za Tanzania pamoja na Makatibu wao.

Akizungumza katika maadhimisho hayo, Mhe. Rais Magufuli ameipongeza BAKWATA na Waislamu wote nchini kwa kuendelea kudumisha amani, umoja, mshikamano na kuyashika vizuri mafunzo ya dini, na amebainisha kuwa mambo hayo yana faida kubwa kwa jamii nzima ya Waislamu na Madhehebu mengine.

Mhe. Rais Magufuli amesema katika kipindi cha miaka 50 taasisi mbalimbali zilizo chini ya BAKWATA na Uislamu kwa ujumla zimeendelea kutoa mchango mkubwa katika maendeleo ya Tanzania kwa kuunga mkono juhudi za Serikali katika utoaji wa huduma za elimu, afya, maji na nyingine na kwamba Serikali inatambua mchango huo mkubwa.

Ameahidi kuwa Serikali ya Awamu ya Tano itaendeleza na kukuza zaidi uhusiano wake mzuri na BAKWATA na Madhehebu mengine ya Dini, na ametoa wito kwa Waislamu na Waumini wa Madhahebu mengine ya Dini kuendeleza utamaduni mzuri wa kushirikiana, kuvumiliana, kusameheana na kutunza amani, mambo ambayo yanasaidia kuepusha migogoro.

“Naomba niwahakikishie ndugu zangu, Serikali inawapenda Waislamu na inayapenda Madhehebu yote ya Dini, tutaendelea kuhakikisha tunashirikiana kulisukuma mbele gurudumu la maendeleo la Taifa letu, kwa pamoja tunaweza” amesema Mhe. Rais Magufuli.

Aidha, Mhe Rais Magufuli ameelezea juhudi mbalimbali zinazofanywa na Serikali kuharakisha maendeleo ikiwemo ununuzi wa ndege, kuanza mradi wa uzalishaji wa umeme katika mto Rufiji, kujenga viwanda, kujenga reli ya kati na kufufua reli ya kaskazini, kujenga meli mpya na kukarabati za zamani, kujenga barabara, kuongeza kasi ya usambazaji umeme vijijini, kujenga hospitali na vituo vya afya na kuongeza ukusanyaji wa kodi.

Amempongeza Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Sheikh Aboubakar Zubeir bin Ally kwa uongozi wake mzuri wa BAKWATA, ushirikiano mzuri na taasisi nyingine ikiwemo Serikali na kutojikweza kwake, na pia ametoa mchango wa shilingi Milioni 30 kwa BAKWATA.

Mapema Mufti wa Tanzania Sheikh Aboubakar Zubeir bin Ally amemshukuru Mhe. Rais Magufuli kwa kuungana nao katika maadhimisho hayo, amemshukuru kwa kusaidia kujengwa kwa Msikiti mkubwa wa BAKWATA Jijini Dar es Salaam ambao utakuwa na uwezo wa kuchukua Waumini 9,000 kwa mara moja, na pia kwa juhudi alizoanza kufuatilia na kurejesha mali za Waislamu zilizoporwa.


“Mhe. Rais kwa niaba ya BAKWATA tunakushukuru sana na Waislamu wameridhika sana kwa kuhakikisha Msikiti huu unajengwa na ujenzi wake unaendelea vizuri” amesema Sheikh Aboubakar Zubeir bin Ally.


Katika Maadhimisho hayo Mhe. Rais Magufuli pia amekabidhi tuzo kwa Waislamu waliotoa mchango mkubwa katika BAKWATA.


Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es Salaam
17 Desemba, 2018

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527