MSAJILI AWATAKA WANASIASA KUACHA UTOTO...MALALAMIKO YAO YANA SABABU ZA PORINI

Baada ya muungano wa vyama 10 vya upinzani kutoa tamko lao la pamoja kupinga maamuzi ya ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa ya kusitisha vikao vya baraza la vyama vya siasa bila kujulisha, ofisi hiyo imeibuka na kujibu tuhuma hizo.

Ofisi hiyo ya Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, imewataka viongozi hao kuacha utoto wa kukwepa wajibu wao wa kuwasiliana na ofisi hiyo, pale wanapoona kuna jambo linawatatiza badala ya kukimbilia katika vyombo vya habari.


Akijibu tuhuma hizo kwa niaba ya Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi, Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa, Sisty Nyahoza, amesema, viongozi hao wa upinzani wanakwepa wajibu wao wa msingi kwa kufanya siasa nyepesi isiyoakisi maana mzima ya kukuza demokrasia nchini.


“Sasa hao wanaosema hawakuwashirikishwa wanataka ushirikishwaji wa namna gani,” amehoji Nyahoza.

Amesema kanuni ya baraza hilo linaruhusu kuahirishwa kwa kikao pale panapokuwa na sababu na uamuzi huo hufanyika baada ya majadiliano na Mwenyekiti wa baraza la vyama.

Nyahoza amesema Katibu wa baraza ambaye ni Msajili, aliwasiliana na Mwenyekiti wa baraza kisha wajumbe wakataarifiwa kwa simu na kwengine kwa njia ya mdomo kwa kuwa kanuni zinaeleza jambo hilo.


"Tumesikia malalamiko yao mengi hayana msingi, ni sababu za porini kwa kuwa ofisi yetu ipo wazi walipaswa kuja kupata ufafanuzi kabla ya kwenda kwenye vyombo vya habari na hii kwa kweli imetusikitisha,” ameongeza.


Pia amesema ofisi yake ilishatoa sababu ya kuahirishwa kwa kikao hicho kuwa ni kupisha uchaguzi mdogo wa marudio na kusisitiza kwamba baada ya uchaguzi huo baraza litakutana tena kujadili mambo yao.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527