MBOWE,MATIKO SASA RASMI KULA KRISMASI NA MWAKA MPYA 2019 GEREZANI

Kesi Na. 112/2018 ya uchochezi inayowakabili Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, Mbunge wa Tarime mjini, Ester Matiko na viongozi wengine saba wa chama hicho imeahirishwa leo Desemba 21, 2018 katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu hadi January 3, 2019.

Wakili wa Serikali Mwandamizi, Simon Wankyo akisaidia na wakili Salim Msemo amedai leo Ijumaa Desemba 21, 2018 mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama hiyo, Wilbard Mashauri kuwa kesi hiyo ilikuja kwa ajili ya kutajwa.

Wakili Simon amedai kuwa hawana taarifa ya kinachoendelea mahakama ya juu hivyo wanaomba tarehe nyingine kwa ajili ya kutajwa.

Hata hivyo, wakili Faraja Mangula amedai kuwa wakili wa washitakiwa hao Peter Kibatala na Sheck Mfinanga wamepata dharura hivyo wanaomba mahakama ipange Januari 4, 2019.

Akijibu hoja hiyo, wakili Simon amedai wanaiachia mahakama ipange tarehe itakayoona inafaa na hakimu Mashauri kuahirisha kesi hiyo hadi Januari 3, 2019.

Mbowe na Matiko wako gereza la Segerea baada ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwafutia dhamana Novemba 23, 2018 kwa kukiuka masharti ya dhamana ikiwemo kutoka nje ya nchi bila kibali.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527