ANAYETUHUMIWA KUUA MTOTO WAKE AACHIWA HURU

Mahakama Kuu Tanzania Kanda ya Tabora, imemwachia huru mkazi wa Kijiji cha Minyinya Wilaya ya Kibondo, Ester Ndalaba (40), baada ya upande wa mashtaka kushindwa kuthibitisha kosa la mauaji ya mtoto mwenye umri wa miaka 8.

Akisoma hukumu hiyo, Jaji wa Mahakama hiyo, Julius Mallaba, alisema mshtakiwa huyo alikuwa ameshtakiwa kwa kosa la kumuua mtoto wake Magreth Gaudes kwa kumkata shingoni na kitu chenye ncha kali kwa kukusudia.

Upande wa mashtaka ulikuwa ukiongozwa na wakili wa serikali, Antia Julius, ambao ulipeleka mahakamani mashahidi watano na vielelezo viwili.

Jaji alisema upande wa mashtaka umeshindwa kuthibitisha kosa hilo la mauaji, hivyo mahakama imemwachia huru mshtakiwa kwa sababu jukumu kubwa la kuthibitisha kosa dhidi ya mshtakiwa ni upande wa mashtaka na kama kuna upande wowote ambao haujaridhika na hukumu hiyo wakate rufani katika mahakama ya rufani.

Upande wa utetezi uliongozwa na wakili wa kujitegemea, Iginatus Kagashe.

Jaji Mallaba alisema mtoto huyo alikuwa ni wa mshtakiwa na alikuwa ni mlemavu wa kuongea, kutotembea na mikono na hadi kifo chake alikuwa na umri wa miaka 8 bila ya kuongea wala kutembea.

Alisema siku ya tukio Mei 4, mwaka 2010 ndipo alipofariki dunia kwa kukatwa shingoni na kitu chenye ncha kali.

Alisema mshtakiwa huyo alihusishwa na kitendo hicho cha mauaji kutokana na kifo cha mtoto huyo kuuawa kwenye chumba cha mshtakiwa huyo.

Credit: Nipashe

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527