KIONGOZI WA TFF AFARIKI DUNIA

Shirikisho la soka nchini TFF limetangaza kifo cha aliyekuwa mtunza vifaa msaidizi wa timu ya taifa 'Taifa Stars', Kessy Rajab kilichotokea jana Desemba 23.








Taarifa ya TFF iliyotolewa na Rais wake, Wallace Karia imesema, "Rais wa Shirikisho la Mpira wa miguu Tanzania TFF Wallace Karia amepokea kwa mshtuko na majonzi makubwa kifo cha aliyekuwa mtunza vifaa msaidizi wa timu ya Taifa ya Tanzania 'Taifa Stars' Kessy Rajab".

"Kwa niaba ya TFF, Rais Karia ametuma salamu za rambirambi kwa familia ya Kessy, ndugu, jamaa, marafiki na watumishi wenzake, " imeongeza taarifa hiyo.

Msiba upo nyumbani kwake, Kurasini karibu na Uhamiaji wakati taratibu nyingine za mazishi zikiendelea.

Kwa mujibu wa taarifa za awali, zinaeleza kuwa chanzo cha kifo hicho ni mshtuko alioupata katika mchezo wa Klabu Bingwa Afrika, kati ya Simba na Nkana Red Devils uliopigwa katika uwanja wa taifa jijini Dar es salaam.

Rajab Kessy alikuwa ni shabiki mkubwa wa Simba na alihudhuria katika mchezo huo wa jana ambao alipata mshtuko mara baada ya Simba kufungwa bao la kwanza. Alikimbizwa hospitali ya Temeke ambako ndiko alipoteza maisha.

Katika mchezo huo, Simba iliibuka na ushindi wa mabao 3-1 na kufuzu hatua ya makundi ya michuano ya Klabu Bingwa Afrika.

Chanzo: Eatv

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527