WAZIRI NDALICHAKO AZINDUA MWONGOZO NA MASHINDANO YA UBUNIFU JIJINI DODOMA


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akimkabidhi Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge na Huduma za Maendeleo ya Jamii Peter Serukamba Mwongozo wa ubunifu mara baada ya kuuzindua leo Jijini Dodoma.
Wakuu wa taasisi zilizo chini ya Wizra ya Elimu na Teknolojia wakifurahia mara baada ya Mwongozo na Mashindano ya ubunifu kuzinduliwa
Waziri Wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako pamoja na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge na Huduma ya Maendeleo ya Jamii Mhe. Peter Serukamba wakionesho mwongozo wa Ubunifu mara baada ya Kuzinduliwa leo Jijini Dodoma.
Waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia Prof.Joyce Ndalichako akimkabidhi mmoja wa wanafunzi kutoka shule ya Sekondari Dodoma Mwongozo wa ubunifu mara baada ya kuzinduliwa leo jijini Dodoma

............................ 

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako leo amezindua mwongozo na mashindano ya ubunifu kitaifa mkoani Dodoma.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo ya uzinduzi Waziri Ndalichako amesema lengo la mashindano hayo ni kutambua na kuendeleza fikra za wabunifu kwa lengo la kuongeza ajira.

Prof. Ndalichako amesema katika kuimarisha uchumi wa viwanda lazima matumizi ya Sayansi, Teknolojia na ubunifu yaimarishwe kwa lengo la kuongeza tija viwandani na kwenye biashara.

“Kutoka na umuhimu wa mashindano haya naielekeza Idara ya Sayansi, Teknolojia na ubunifu kuhakikisha mashindano haya yanafanyika kila mwaka, ili kukuza ujuzi, wabunifu kwa maendeleo ya viwanda,” alisisitiza Waziri Ndalichako.

Mashindano hayo yameshirikisha Makundi mbalimbali ya kijamii zikiwemo Shule za Sekondari, Vyuo vya Ufundi Stadi, Sekta isiyo rasmi, Vyuo vya ufundi wa Kati, Vyuo vya Elimu ya Juu na Taasisi za utafiti na Maendeleo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Maendeleo ya Jamii Mhe. Peter Serukamba amesema kuwa kuzinduliwa kwa mwongozo huo ni jambo kubwa na la kihistoria ikizingatiwa kuwa nchi inaelekea kwenye uchumi wa viwanda.

Serukamba amesema bila Sayansi, Teknolojia na ubunifu nchi haiwezi kufanikisha malengo yake, hivyo ameiomba Serikali ihakikishe inawekeza fedha nyingi.

“Kama hatutawekeza fedha za kutosha kwenye Sayansi, Teknolojia na Ubunifu hatuwezi kufanya kitu, hivyo tuwekeze fedha za kutosha ili tujiletee Maendeleo kwa haraka,” amesema Mhe. Serukamba.

Kauli mbiu ya mashindano hayo ni “Kukuza Ujuzi na Ubunifu kwa Uchumi wa Viwanda.”

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527