SPIKA NDUGAI AWAPIGA KIJEMBE WAPINZANI...AWATAKA WAVUMILIE SINDANO


SPIKA wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai leo tarehe 15 Novemba 2018 akiwa bungeni jijini Dodoma, amewatania wabunge wa upinzani akiwataka kuvumilia kuona wabunge waliohamia CCM wakitokea kwenye vyama vyao, wakisimama bungeni. 


Spika Ndugai ametoa kauli hiyo baada ya Mbunge wa Babati mjini aliyetokea Chadema na kuhamia CCM kwa ajili ya kuunga mkono juhudi za Rais John Magufuli, Pauline Gekul kuuliza swali, ambapo aliwapa pole watani zake na kuwataka wavumilie kitendo hicho alichokiita kuwa ni sindano.

“Watani zangu poleni sana leo mvumilie tu hii sindano,” amesema Spika Ndugai.

Kabla ya kutoa kauli hiyo, Spika Ndugai amesema amemuona Mbunge wa Iringa Mjini kupitia Chadema, Mchungaji Peter Msigwa, ina muuma sana.

Ndugai amesema hayo baada ya Joseph Mkundi, Mbunge wa Ukerewe aliyehamia CCM akitokea Chadema ambacho ni chama cha Msigwa, kwa mara ya kwanza kusimama bungeni kwa ajili ya kuuliza swali.

Vyama vya upinzani hivi karibuni vilikutana na changamoto ya kukimbiwa na baadhi ya wabunge, madiwani na viongozi wake, waliohamia CCM kwa sababu mbalimbali ikiwemo kuunga mkono juhudi za serikali ya awamu ya tano kufuatia kuridhishwa na utendaji kazi wa awamu hiyo.

Chanzo- Mwanahalisi online

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527