LOWASSA AMPONGEZA MAGUFULI KWA KAZI NZURI....

Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa amempongeza Rais John Magufuli kwa utendaji wake mzuri wa kazi.

Kauli hiyo ya Lowassa ni ya pili kuitoa tangu kumalizika kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.

Mara ya kwanza ilikuwa Januari 2018 alipofanya mazungumzo na Rais Magufuli Ikulu Dar es Salaam na kumsifu kwa kazi anazoendelea kuzifanya, ikiwa ni pamoja na miradi ya maendeleo, elimu na ajira na pia mkuu huyo wa nchi akamsifia mbunge huyo wa zamani wa Monduli kwa kuendesha siasa za kistaarabu.

Leo Jumanne Novemba 27, 2018 Lowassa ametoa tena pongezi hizo baada ya Magufuli kumualika katika uzinduzi wa maktaba ya kisasa ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).

“Mheshimiwa Rais asante kwa mwaliko, asante kwa kufanya vizuri, ahsanteni sana,” amesema Lowassa kwa kifupi.

Mara ya kwanza viongozi hao walikutana Agosti 28, 2016 ikiwa ni miezi 16 tangu Lowassa alipohamia Chadema kupinga mchakato wa kumpata mgombea urais wa CCM ulioishia Magufuli kupitishwa.

Siku hiyo walikutana kwenye misa ya shukrani ya kuadhimisha miaka 50 ya ndoa ya Rais wa Serikali ya Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa iliyofanyika Kanisa Katoliki la Mtakatifu Petro lililopo Oysterbay jijini Dar es Salaam.

Leo, mbali na Lowassa wageni wengine waliopewa nafasi ya kusalimu katika uzinduzi huo ni Jaji Mkuu wa Tanzania, Profesa Ibrahim Juma, Jaji mstaafu Joseph Warioba, Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Profesa Florens Luoga, Waziri wa Katiba na Sheria, Profesa Palamagamba Kabudi na Mwenyekiti wa Baraza la UDSM, Jaji mstaafu Damian Lubuva. 

Maktaba hiyo imejengwa na Serikali ya China kwa gharama ya Sh90 bilioni, wanafunzi 2,100 wanaweza kuitumia kwa wakati mmoja. Ina vitabu 800,000 na ukumbi wa mikutano wenye uwezo wa kuchukua watu 600.




Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527