MBUNGE ALIYEGOMA KUHAMIA CCM AFUNGUKA...ADAI KUMPELEKA CCM NI SAWA NA KUPELEKA BAHARINI ASIYEJUA KUOGA


Mbunge wa Chama Cha Wananchi CUF Katani Ahmed Katani.

Mbunge wa Chama Cha Wananchi CUF Katani Ahmed Katani, ameendelea kueleza msimamo wake wa kutohama Chama Chake wananchi CUF, kwa kile alichokidai yeye ni miongoni mwa waathirika wakubwa wa utawala wa Chama Cha Mapinduzi.

Kwa mujibu wa Mbunge huyo wa Tandahimba, amedai kuwa kabla hajagombea ubunge, alishawahi kuwekwa ndani na serikali ya Chama Cha Mapinduzi kwa hiyo hata siku moja hataweza kuhamia chama hicho.

“Watu wengi wasichokijua siasa za upinzani Tandahimba ziko kwenye damu, kunipeleka mimi CCM ni sawa na kumpeleka baharini mtu ambaye hajui kuoga, unaponirudisha niende chama fulani ili itumike bilioni 1 kwa ajili ya uchaguzi wa marudio wakati kwenye jimbo langu kuna matatizo nipe nifanye maendeleo.” Amesema Katani.

“Mimi nilianza kugombea ubunge tangu 2010 lakini nipo kwenye harakati kila siku, nilivunjwa mkono uchaguzi 2010 kwa hiyo mimi nimepata tabu kwenye siasa za upinzani, najua na naelewa machungu ya tunachopigania kama wanasiasa wa upinzani.” Ameongeza Katani.

Katani alikuwa ni swahiba mkubwa wa aliyekuwa Mbunge wa Temeke Abdallah Mtolea ambaye alikuwa ni Mbunge wa Temeke na baadaye kuhamia CCM kwa kile alichokieleza kuchoshwa na mgogoro wa kiuongozi kwenye chama chake.

Chanzo- EATV

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527