BABU WA MIAKA 65 MATATANI KWA TUHUMA YA KUBAKA MTOTO WA MIAKA MITATU

Mkazi wa Mburahati Motomoto, jijini Dar es Salaam, Mohamed Hassani (65) anashikiliwa na jeshi la polisi mkoa wa Kinondoni akituhumiwa kumbaka mtoto wa kike wa miaka mitatu.



Mama mlezi wa mtoto huyo, Hadija Saidi amesema siku ya tukio mtuhumiwa alimwita mwanaye kwenye chumba chake ili amtume dukani na alimwandikia kwenye karatasi dawa ya Diclopre na pipi ili akanunue.


Amesema hawakuwa na wasiwasi naye kwa kuwa mtuhumiwa alikuwa mtu mzima na mara nyingi amekuwa akimwita mtoto huyo ndani kwake na wakati mwingine akimtuma dukani.


"Huyu mzee ni mpangaji mwenzetu, hana mke na tulikuwa tunamheshimu sana wapangaji wote na tunamuita mjomba kutokana na uzee wake yaani sikuamini siku hiyo napigiwa simu na mpangaji mwenzangu akiniambia nirudi haraka nyumbani nikamwangalie mtoto amebakwa," amesema Hadija.


Hadija anasema wameshafungua jalada la kesi ya ubakaji yenye namba MBT/RB/5395/2018 ambapo mtuhumiwa ameshakamatwa hivyo wanasubiri afikishwe kwenye vyombo vya sheria.


Kamanda wa polisi mkoa wa Kinondoni, Jumanne Muliro amesema tukio hilo lilitokea Oktoba 31, 2018 maeneo ya Mburahati Motomoto ambapo mtuhumiwa alimfanyia mtoto huyo kitendo akiwa kwenye chumba chake.


"Taarifa za kubakwa mtoto huyo tunazo tunazishughulikia kwa mujibu wa sheria na tutahakikisha mtuhumiwa anafikishwa mahakamani," amesema Muliro,

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527