Picha : AGPAHI YATOA MSAADA WA MAGARI KUBORESHA UTOAJI HUDUMA ZA VVU NA UKIMWI MWANZA

Asasi ya Ariel Glaser Pediatric AIDS Health Initiative (AGPAHI) inayolenga kutokomeza UKIMWI kwa watoto na familia nchini Tanzania imetoa msaada wa magari mawili aina ya Nissan Patrol kwa halmashauri za wilaya za Buchosa na Misungwi mkoani Mwanza kwa ajili ya kuboresha utoaji wa huduma za VVU na UKIMWI katika halmashauri hizo.

Magari hayo yenye namba za usajili DFPA 7015 na DFPA 7016 yana thamani ya shilingi milioni 186 yamenunuliwa na shirika la AGPAHI kwa ufadhili wa Watu wa Marekani kupitia Mfuko wa Dharura wa Rais wa Marekani wa Kupambana na UKIMWI (PEPFAR) chini ya vituo vya Kudhibiti Magonjwa na Kinga (CDC).

Hafla fupi ya Makabidhiano ya magari, imefanyika leo Jumatatu Novemba 5,2018 wakati wa kikao cha wadau wa afya na ustawi wa jamii mkoa wa Mwanza kilichofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Gold Crest jijini Mwanza ambapo mgeni rasmi alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mheshimiwa John Mongella.

Akizungumza wakati wa kukabidhi magari hayo kwa Mkuu huyo wa mkoa, Mkurugenzi Mtendaji wa AGPAHI, Dkt. Sekela Mwakyusa alisema msaada huo wa magari ni kwa ajili ya kuboresha utoaji huduma za afya hususani za VVU na UKIMWI kwenye vituo vya kutolea huduma.

Dkt. Mwakyusa alisema, AGPAHI imekuwa ikifanya kazi kwa karibu na halmashauri katika kuboresha huduma za VVU na UKIMWI kwa ajili ya ustawi wa wananchi na taifa kwa ujumla.

“Magari tuliyokabidhi leo yana thamani ya shilingi milioni 186, na hii ni sehemu ya vyombo vya usafiri (magari,pikipiki na baiskeli) vyenye thamani ya shilingi milioni 900.2 tulivyonunua katika kipindi cha kuanzia Oktoba 2017 hadi Septemba 2018 kwa ajili ya kuleta tija kwenye utendaji kazi ili kuboresha huduma za VVU na UKIMWI katika halmashauri ambazo AGPAHI inafanya kazi,” alieleza Dkt. Mwakyusa.

Aliongeza kuwa katika jitihada za kuboresha utoaji wa huduma za VVU na UKIMWI, katika kipindi hicho, AGPAHI imefanyia ukarabati vituo 146 vya kutolea huduma vikiwemo 36 vya mkoa wa Mwanza. Pia imeweka mifumo ya umeme jua kwenye vituo 40 vya kutolea huduma kwenye halmashauri mbalimbali.

Akipokea magari hayo, Mkuu wa mkoa, Mheshimiwa Mongella aliishukuru AGPAHI kwa kuwa mdau muhimu katika sekta ya afya na kuomba waendelee kushirikiana na serikali katika kuboresha huduma za afya kwa wananchi.

Mheshimiwa Mongella aliwataka watendaji wa halmashauri zilizopewa magari kutunza na kuyatumia magari hayo kwa kazi za afya na maendeleo ya halmashauri na siyo vinginevyo.

ANGALIA PICHA HAPA CHINI
Mkuu wa mkoa wa Mwanza, Mheshimiwa Mongella, akizungumza wakati wa kikao cha wadau wa afya na ustawi wa jamii mkoa wa Mwanza katika ukumbi wa Hoteli ya Gold Crest jijini Mwanza ambapo kikao hicho kimeenda sanjari na hafla fupi ya AGPAHI kukabidhi magari mawili kwa halmashauri ya wilaya ya Buchosa na Misungwi.Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog
Mkurugenzi Mtendaji wa asasi ya AGPAHI, Dkt. Sekela Mwakyusa, akizungumza wakati wa kukabidhi magari mawili kwa mkuu wa mkoa wa Mwanza, Mheshimiwa John Mongella kwa ajili ya halmashauri ya wilaya ya Buchosa na Misungwi ili kuboresha huduma za VVU na UKIMWI katika vituo vya kutolea huduma. Kushoto ni Mganga Mkuu wa mkoa wa Mwanza, Dkt. Thomas Rutachunzibwa.
Mkuu wa mkoa wa Mwanza,Mheshimiwa John Mongella, akiishukuru AGPAHI kwa kutoa msaada wa magari huku akiahidi kuwa magari hayo yatatumika kwa lengo lililokusudiwa na kuboresha huduma za VVU na UKIMWI.
Magari yenye namba za usajili DFPA 7015 na DFPA 7016 yenye thamani ya shilingi milioni 186 yaliyonunuliwa na shirika la AGPAHI kwa ufadhili wa Watu wa Marekani kupitia Mfuko wa Dharura wa Rais wa Marekani wa Kupambana na UKIMWI (PEPFAR) chini ya vituo vya Kudhibiti Magonjwa na Kinga (CDC).
Mkuu wa mkoa wa Mwanza, Mheshimiwa John Mongella, akikata utepe wakati wa hafla ya makabidhiano ya magari yaliyotolewa na AGPAHI kwa ajili ya kuboresha huduma za VVU na UKIMWI katika halmashauri ya wilaya ya Buchosa na Misungwi mkoani Mwanza.
Kulia ni Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Buchosa,Crispin Luanda na Mkuu wa mkoa wa Mwanza, Mheshimiwa John Mongella (wa tatu kulia) wakioneshana magari yaliyotolewa na AGPAHI.
Muonekano wa magari yaliyotolewa na AGPAHI kwa ajili ya kuboresha huduma VVU na UKIMWI katika halmashauri ya wilaya ya Misungwi na Buchosa.
Mkurugenzi Mtendaji wa AGPAHI, Dkt. Sekela Mwakyusa, akikabidhi ufunguo wa gari kwa Mkuu wa mkoa wa Mwanza, Mheshimiwa John Mongella.
Mkuu wa mkoa wa Mwanza, Mheshimiwa John Mongella, akionesha ufunguo wa gari.
Mkurugenzi Mtendaji wa AGPAHI, Dkt. Sekela Mwakyusa, akikabidhi kadi ya gari kwa Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Misungwi, Mheshimiwa Anthony Bahebe.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Buchosa,Crispin Luanda akipokea ufunguo wa gari.
Watumishi wa Halmashauri ya wilaya ya Buchosa wakiangalia gari walilokabidhiwa.
Dereva wa halmashauri ya wilaya ya Misungwi ,Nicholaus Mzee, akiwa ndani ya gari walilokabidhiwa.
Muonekano wa magari yaliyotolewa na AGPAHI.
Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527