MKUU WA MKOA AWATAKA WAGANGA WA KIENYEJI KUFUFUA MAITI MBEYA


Mkuu wa mkoa wa Mbeya, Albert Chalamila amewataka waganga wa kienyeji maarufu kama lambalamba mkoani humo kwenda kuwafufua watu waliofariki dunia, ndipo atakapowaruhusu kuendelea na kazi yao ya kutoa uchawi.

Akizungumza na mwandishi wa www.eatv.tv, Mh. Chalamila amesema kwamba ameamua kutoa agizo hilo baada ya wananchi kumuomba awaruhusu waganga hao kufanya kazi yao ya kutoa uchawi, jambo ambalo serikali haiamini.

“Walileta maombi maalum kuwa serikali iwaruhusu huku wakitoa ushuhuda watu hao wakitoa uchawi, kutoa baadhi ya vitu na kuponya watu, ndipo mimi niliposimama nikasema haitawezekana, nikawaambia kama mnawashukuru wanaowaponya, nitawaruhusu kwa masharti, tukutane nao mochwari katika hospitali ya rufaa ya Mbeya, wanifufulie maiti zilizopo pale, kwa ushuhuda huo nitawaruhusu kweli ni waponyaji katika ulimwengu wa roho”, amesema Chalamila.

Mh. Chalamila aliendelea kwa kusema kwamba iwapo watu hao wataweza kufanya kazi zao kisayansi yenye kuleta manufaa, hatosita kuwaruhusu kuendelea kufanya shuhuli zao zenye imani ya kishirikina.

"Mimi nataka kwa sayansi, wakinisaidia hilo nitawaruhusu, kwa mfano mtu anataka kuwahi Dar es salaam wakanionyesha nitakubali, au walete mvua wakati wa kiangazi tumwagilie mazao yetu, wanaopotea waseme wako wapi, mimi nataka hilo”, amesema Mh. Chalamila.
Chanzo - EATV

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527