TCU YAONGEZA KWA MARA NYINGINE KWA WANAOOMBA VYUO VIKUU

Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU), imefungua dirisha la udahili kwa mara ya nne kwa waombaji ambao hawakuchaguliwa katika awamu zilizopita.

Kwa mujibu wa taarifa iliyowekwa kwenye tovuti ya TCU, iliyotolewa na Katibu Mtendaji, ilieleza kuwa udahili huo ni kwa wanafunzi wanaotaka kujiunga na vyuo vikuu kwa mwaka wa masomo 2018/19.


Aidha, taarifa hiyo ilieleza kuwa udahili ulianza Oktoba 13 na utaendelea hadi 20, mwaka huu.


“Waombaji wapya na wale ambao hawakuchaguliwa katika awamu zilizopita wanahimizwa kutumia fursa hii ya mwisho kutuma maombi yao ya udahili moja kwa moja kwenye vyuo na taasisi za elimu ya juu nchini,” ilifafanua taarifa hiyo.


Aidha, taarifa hiyo ilibainisha kuwa waombaji wote wanakumbushwa kuomba programu ambazo wanakidhi vigezo kama ilivyoelekezwa katika kitabu cha mwongozo wa udahili na kwamba tume inaelekeza vyuo na taasisi za elimu ya juu kutangaza programu ambazo bado zina nafasi na idadi ya nafasi zilizobaki ili waombaji waweze kutuma maombi yao.


Hivi karibuni, TCU iliwataka waombaji wote wa vyuo waliochaguliwa kwenye chuo zaidi ya kimoja, kuthibitisha udahili wao na mwisho ilikuwa Oktoba 5, mwaka huu.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527