MBAO FC SIYO WA KUBEZA..WAMEICHAPA SIMBA SC CCM KIRUMBA


Kikosi cha Mbao FC.

Hatimaye Mbao Fc imevua uteja kwa Simba baada ya kuichapa kwa bao 1-0 katika mechi kali ya ligi kuu soka Tanzania bara iliyopigwa kwenye uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza na kukamata usukani wa ligi.


Bao pekee lililozamisha jahazi la Simba lilisukumiziwa kimiani na Said Said kwa mkwaju wa penati kufuatia makosa ya mlinda mlango, Aishi Manula kumwangusha mshambuliaji wa Mbao, Pastore Athanas aliyekuwa akielekea kupachika bao.

Hiki ni kipigo cha kwanza kwa mabingwa hao watetezi katika msimu huu na kuendeleza mwenendo usioridhisha wa mechi za ugenini baada ya kutoka sare na Ndanda Fc katika uwanja wa Nangwanda Sijaona mkoani Mtwara wikiendi iliyopita.

Matokeo haya yanazidisha hofu kwa wanachama wa Simba kuelekea kwenye mechi ya watani wa jadi dhidi ya Yanga itakayopigwa Septemba 30 mwaka huu huku kukitajwa kuwepo kwa mgogoro ndani ya klabu hiyo ikiwahusisha makocha.

Licha ya kutumia silaha zote za maangamizi wakiwemo nyota wao Emmanuel Okwi,John Bocco,Shiza Kichuya na Meddie Kagere aliyetokea benchi kuchukua nafasi ya Mohamed Ibrahim lakini safu ya ushambuliaji ya mnyama ilishindwa kufurukuta kwa vijana wa .

Ushindi huo wa Mbao Fc ni wa kwanza dhidi ya Simba katika michezo yote waliyokutana tangu ilipopanda ligi kuu misimu miwili iliyopita, ambapo sasa inaongoza ligi kwa alama 10 baada ya kushuka dimbani michezo mitano.

Matokeo ya michezo mingine ni, Mtibwa Sugar ililazimishwa sare ya 2-2 ugenini dhidi ya Tanzania Prisons, Singida United ikichapwa mabao 3-2 na wenyeji African Lyon katika uwanja wa taifa.
Via>>EATV

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527