TUNDU LISSU KUREJEA TANZANIA

Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu hatafanyiwa upasuaji mwingine na ataendelea kubaki na risasi moja kwenye uti wa mgongo.

Hayo yameelezwa leo Agosti 29 na kaka yake Lissu, Wakili Alute Lissu, alipozungumza na wanahabari.

Amesema Lissu hatafanyiwa upasuaji mwingine baada ya kufanyiwa upasuaji zaidi ya mara nne akiwa Ubelgiji ingawa kuna risasi moja ambayo bado imebaki nyuma ya uti wa mgongo.

“Wakijaribu kuitoa huenda ikaathiri uti wa mgogo na hivyo kupata tatizo la kupooza,"amesema.

Lissu alihamishiwa hospitali ya Leuven iliyopo Ulelgiji akitokea hospitali ya Nairobi, baada ya kushambuliwa kwa risasi kadhaa na watu wasiojulikana Septemba 7 mwaka jana.

Alute ambaye amerejea nchini, wiki hii akitokea Ubelgiji kumjulia hali Lissu, amesema huenda mwanasiasa huyo akarejea nchini mwakani, hasa kutokana na mfupa wa mguu wa kulia kuwa bado haujaunga vizuri.

"Hali ya Lissu inaendelea vizuri, lakini napenda kukanusha taarifa kuwa kuna kamati ya mapokezi yake kwani, Lissu kwa hali yake hawezi kurejea nchini hivi karibuni, kutokana na kuendelea na matibabu nje ya hospitali,’’ amesema.

Wakili Mughwai amesema bado Lissu hajapata ruhusa ya moja kwa moja kutoka kwa daktari wake hivyo atakuwa akipatiwa huduma kwenye nyumba aliyopanga jirani na hospitali hiyo ya Chuo Kikuu cha Leuven nchini Ubelgiji.

"Haiwezekani kurudi karibuni, mimi nadhani labda mwakani hasa kutokana na kuhitaji uangalizi wa daktari wake, ingawa yeye binafsi na hata sisi wanafamilia tungependa arudi mapema,"amesema.

Amesema risasi hiyo imeachwa kwa sababu haina athari kwa maisha ya Lissu, kwani si mara ya kwanza, wagonjwa kubaki na risasi mwilini kwani itasababisha madhara makubwa zaidi kama ikitolewa.

Hata hivyo, Wakili Mughwai amesema wanashukuru sana Watanzania wote wakiwepo wanaoishi Ubelgiji kutokana na michango wanayotoa kumsaidia Lissu na kwenda kumjulia hali nchini Ubelgiji.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527