MKURUGENZI MKAZI UNDP ALETA HERI SAME


Mkurugenzi mkazi wa UNDP, Natalie BOUCLY ametembelea Wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro kwa ziara yake ya siku mbili, na kukagua miradi iliyofadhiliwa na UNDP kupitia shirika la SIPRO na TFS.

Katika ziara yake hiyo, Bi. Boucly alibidhi majengo 4 yaliyojengwa kupitia mradi wa Kuboresha usimamizi wa Misitu ya Mazingira Asilia na kukuza utalii kwa ufadhili wa UNDP kwa TFS, Majengo yaliyojumuisha ofisi ya msitu wa Chome na ofisi 3 (ranger outposts) kwa ajili ya usimamizi wa msitu katika kata ya Chome, Bwambo na Bombo. 

Mradi huo pia umejenga majengo kama hayo katika misitu sita nchini ambayo ni Minziro, Uzdungwa, Mt Rungwe, Magamba na Mkingu. Baadaye alitembelea mradi wa ujenzi wa Daraja Heikapombe kata ya Makanya na mradi wa jengo la kijiji cha Mhero kata ya Chome.

Naye Mtendaji Mkuu wa TFS, Prof. Dos Santos Silayo aliyeambatana naye aliahidi kuendelea kuimarisha utalii katika hifadhi ya Chome kama ilivyo kipaumbele cha serikali katika hifadhi zote za misitu nchini.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Same, Rosemary Senyamule, alitoa shukrani kwa UNDP na kuwaahidi usimamizi makini wa fedha zote zinazotolewa, pia aliwakumbusha TFS kuongeza tija kwa miradi inayotolewa kwa wananchi wa vijiji 27 vinavyozunguka msitu wa TFS kama mbadala sahihi na kuongeza utayari wa wananchi kulinda msitu huo.

"Nategemea tukiimarisha utalii kwenye eneo la Shengena, tutawashirikisha wananchi wengi wawe sehemu ya utalii huo. Wakiona tija ya utalii, wataulinda msitu wetu ambao ni kama moyo wa Wilaya ya Same" . Alisema DC Huyo.

Ziara ya viongozi hao ilifanyika Tar. 20 na 21 Aug. 2018. Ambapo pia walikuwepo wawakilishi toka wizara ya Fedha na TAMISEMI .

Mkuu wa Wilaya ya Same, Rosemary Senyamule akimkabidhi sehemu ya zawadi, Mkurugenzi mkazi wa UNDP, Natalie Boucly alipomtembelea ofisini kwake.
Mkurugenzi mkazi wa UNDP, Natalie Boucly akiwasilikiza baadhi ya wananchi wakati alipotembelea kijiji cha Mhero kata ya Chome.
Mapunziko baada ya ziara ndefu.
Moja ya majengo 4 yaliyojengwa kupitia mradi wa Kuboresha usimamizi wa Misitu ya Mazingira Asilia na kukuza utalii kwa ufadhili wa UNDP kwa TFS

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527