BABA AUA MWANAE KWA KIPIGO KISA KWANINI HAJAHUDHURIA SHULENI


Kamanda wa Polisi Mwanza, Ahmed Msangi.

Mwanafunzi wa kidato cha nne katika Shule ya Sekondari ya Kata ya Sumbugu wilayani Misungwi jijini Mwanza, Mariamu Tabu (18)amefariki dunia kwa kile kilichodaiwa ni kupigwa na baba yake mzazi baada ya kutohudhuria shuleni.

Akizungumza na wanahabari leo Agosti 9,2018 Kamanda wa Polisi mkoa wa Mwanza Ahmed Msangi amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba mtuhumiwa anashikiliwa na polisi kituo cha Misungwi na atafikishwa mahakamani kujibu mashtaka.

Kamanda Msangi amesema kuwa mama mzazi wa Mariam, Kija Mashauri amelieleza Jeshi la Polisi kuwa Agosti 6, mwanaye alikwenda shule lakini hakurudi nyumbani badala yake alirudi Agosti 7 jioni, ndipo baba yake aliuliza alipokuwa na kuanza kumpiga.

“Baba tayari tumemkamata kwa ushirikiano na wananchi, mara baada ya kutekeleza tukio la kumuua mwanae alitaka kukimbia akazuiwa na wanakijiji, ambapo walimuwahisha mtoto katika zahanati ya kijiji kwakuwa alikuwa katika hali mbaya alifariki akiwa mapokezi”, amesema Msangi.

Juni 16, 2018 katika kilele cha siku ya Mtoto wa Afrika, ambayo kitaifa ilifanyika mkoani Arusha ambapo Tanzania ikitajwa kuongoza katika vitendo vya ukatili dhidi ya watoto kuliko uovu unaofanywa kwenye ujambazi, takwimu zilizowasilishwa na Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto , Dkt. Faustine Ndugulile, zinaeleza kuwa watoto 41,000 walifanyiwa ukatili katika kipindi cha kuanzia mwaka 2012 hadi sasa, na kati yao 3,467 waliripotiwa kuanzia Januari hadi Disemba 2017.

Lakini pia, Idara ya Ustawi wa Jamii wizarani hapo, ilieleza kuwa asilimia 60 ya ukatili dhidi ya watoto unafanyika nyumbani, asilimia 33 ni shuleni na iliyobaki ni maeneo mengine.

Chanzo- EATV

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527