VIONGOZI WAMIMINIKA MUHIMBILI KUMUONA WAZIRI KIGWANGALLA


Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Hamisi Kigwangalla akiwa ndani ya gari la wagonjwa kwa ajili ya kupelekwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa ajili ya matibabu mara baada ya kuwasili katika uwanja wa ndege wa Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es Salaam. 
***

Mawaziri mbalimbali wamefika katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kumjulia hali Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk Hamisi Kigwangalla aliyepata ajali leo asubuhi Jumamosi Agosti 4, 2018.

Dk Kigwangalla amepata ajali eneo la Magugu mkoani Manyara na kupata majeraha sehemu mbalimbali mwilini.

Awali, waziri huyo alipatiwa matibabu katika kituo cha afya cha Magugu na kuhamishiwa hospitali ya Arusha Lutheran Medical Center kwa helkopta na kisha Muhimbili.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega alikuwa wa kwanza kufika hospitalini hapo na kufuatiwa na naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Ashatu Kijaji na naibu Waziri wa Mambo ya Nje, Dk Suzan Kolimba.

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Hamadi Masauni aliwasili na viongozi mbalimbali wizara hiyo na ya Maliasili na Utalii.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dk Mpoki Ulisubisya na mkurugenzi mtendaji wa Muhimbili, Profesa Lawrence Museru pamoja na jopo la madaktari walimpokea Dk Kigwangalla katika kitengo cha magonjwa ya dharura Muhimbili.

Ndugu, jamaa na marafiki pia walifika hospitalini hapo kumjulia hali waziri huyo ambaye pia ni mbunge wa Nzega Vijijini.
Na Herieth Makwetta, Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527