WAZIRI MKUU AWATAKA WANAUME WOTE KISHAPU KUPIMA AFYA ZAO


Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amewataka wanaume wote wa wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga wakapime afya zao ili kubaini kama wameambukizwa virusi vya UKIMWI au la.

Ametoa rai hiyo wakati akizungumza na mamia ya wananchi wa kijiji cha Mwangongo na vijiji vya jirani kwenye mkutano wa hadhara mara baada ya kukagua soko la pamba kwenye kijiji hicho, wilayani Kishapu mkoani Shinyanga.

“Napenda kusisitiza kwa akina baba wote kwamba ukimwi bado upo na wanaume hamuendi kupima, ni wagumu kwenda kupima eti kwa sababu mnawategemea wake zenu waende kupima”, amesema Majaliwa.

Majaliwa ameongeza kuwa, “Unamwambia mama aende kupima virusi vya UKIMWI akija na majibu ukajua hana maambukizi, wewe huku unashangilia kwamba uko salama. Hapana, nendeni mkapime kwa sababu kila mmoja na vyanzo vyake vya kupata maambukizi”.

Waziri Mkuu amebainisha kuwa maambukizi ya virusi vya UKIMWI (VVU) katika wilaya ya Kishapu yako kwenye asimilia 2.1 ikilinganishwa na kiwango cha maambukizi ya VVU kwa mkoa mzima ambayo kwa sasa ni asilimia tano.

Kwa mujibu wa matokeo ya Utafiti uliotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) katika maadhimisho ya siku ya UKIMWI duniani Disemba 1, 2017 ulionyesha kuwa jumla ya Watanzania milioni 1.4 sawa na asilimia 2.9 wanaishi na virusi vya Ukimwi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527