RONALDO AACHA NAMBA ZA MAAJABU REAL MADRID


Cristiano Ronaldo

Jioni ya leo Julai 10, imeacha historia kubwa katika soka ikirudisha dunia nyuma miaka 9 iliyopita, ambapo Ronaldo alihama kutoka Manchester United kwenda Real Madrid kwa dau la rekodi ya dunia la £84.60m zaidi ya shilingi billioni 220.

Mabingwa wa Italia klabu ya Juventus wamekamilisha usajili wa nyota huyo raia wa Ureno kwa dau la €100 milioni zaidi ya shilingi billioni 267, akitokea Real Madrid ambako amecheza kwa miaka 9 na kujitengenezea namba nyingi za rekodi.

Huenda zikatajwa sana hizi namba mbili 450 na 438 kuliko zingine, lakini ukweli utabaki kuwa mchezaji bora mara tano duniani Cristiano Ronaldo, ameacha namba nyingi ambazo hazitafutika ndani ya mabingwa mara 13 wa Ulaya Real Madrid.

450 ni idadi ya mabao ambayo ameifungia timu hiyo na 438 ni idadi ya michezo ambayo ameichezea timu hiyo. Ronaldo pia ana rekodi ya kufunga mabao 30 na zaidi katika misimu yake 9 aliyoichezea Real Madrid.

17 ni rekodi ya mabao katika msimu mmoja wa ligi ya mabingwa wa 2013/14. 105 ni mabao aliyoifungia Real Madrid kwenye ligi ya Mabingwa Ulaya. 311 ni mabao aliyofunga kwenye La Liga. 16 ni idadi ya mataji ambayo amebeba akiwa na Madrid. 44 ni idadi ya hat-trick alizofunga akiwa Real Madrid. 

Kwa ujumla mpaka sasa Ronaldo ana mabao 659, 5 akiifungia Sporting Lisbon, 118 Manchester United, 451 Real Madrid na 85 Ureno. Akiwa na miaka 33, Ronaldo amesaini mkataba wa miaka minne utakaomalizika Juni 2022 akiwa na miaka 38.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527