MAAFISA WA POLISI WAAMURIWA KUPUNGUZA VITAMBI LA SIVYO WAFUKUZWE KAZI

Idara ya polisi nchini India imewaamuru maafisa wake kupunguza uzito vinginevyo watasimamishwa kazi.

Mkuu wa idara hiyo katika jimbo la Karnataka ameiambia BBC kuwa alikuwa na wasiwasi kuhusu ongezeko la maafisa wenye vitambi

Bhaskar Rao amesema alichukua uamuzi huo baada ya maafisa zaidi ya 100 kupoteza maisha katika kipindi cha miezi 18 iliyopita kutokana na maradhi yaliyo na uhusiano na mtindo wa maisha

Maafisa hao watapatiwa usaidizi kwa ajili ya kubadili mfumo wa maisha na namna ya kula.

Idara ya Polisi katika jimbo hilo lina askari 14,000, ambao hutazama hali ya usalama wakati wa matukio makubwa na kudhibiti maandamano na vurugu.

Maafisa wa juu wa kikosi cha KSRP kimekuwa kikiamriwa kuwatambua maafisa wenye uzito mkubwa na kuwaweka katika mpango wa kufanya mazoezi ili kupunguza uzito

''Tumeanza kazi ya kuwafuatilia maafisa kwa kupima sukari na vipimo vingine miezi sita iliyopita.Hatua hii mpya ya kusimamishwa kazi ni kitisho kwa wale wasiojali afya zao''.Rao aliiambia BBC

Sio kawaida kuwaona Polisi nchini humo wakifanya mazoezi kuondokana na tatizo la uzito mkubwa.

''Katika kipindi cha miezi 18 iliyopita, polisi 153 walipoteza maisha, kati ya hawa, 24 walifariki kutokana na ajali za gari na wengine 9 walijiua.Wengine walipoteza maisha kutokana na maradhi yaliyosababishwa na mtindo wa maisha kama vile maradhi ya moyo na kisukari.Hii ni tahadhari kubwa kwa kikosi''.Alisema Rao

Ameongeza kuwa maafisa walikuwa wakila zaidi vyakula vya kukaanga, walikuwa wakivuta sigara, kunywa pombe na hawakuwa wakifanya mazoezi.

Mafunzo ya kuogelea, Yoga na michezo mingine imeanza kutolewa kwa maafisa.

''Mafunzo yameanza kutolewa baada ya kufanyika vipimo na mazoezi yatafanyika kwa kuzingatia ushauri wa madaktari'', alieleza Rao

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527