JAMBAZI AUAWA KWA KUPIGWA RISASI AKITOROKA POLISI RUKWA

Jeshi la Polisi mkoani Rukwa limemuua kwa kumpiga risasi anayedaiwa kuwa jambazi sugu aliyekuwa akitafutwa kwa muda mrefu katika mikoa tofauti hapa nchini, baada ya kujaribu kutoroka akiwa chini ya ulinzi.


Akitoa taarifa ya tukio hilo jana, Kamanda wa Polisi mkoani humo, George Kyando, alimtaja jambazi huyo kuwa ni Patrick Steven (41), maarufu kwa jina la Kamagali, ambaye aliuawa katika eneo la Kashai kata ya Senga katika Manispaa ya Sumbawanga.


Alisema kuwa Julai 15, mwaka huu majira ya saa 12:45 jioni, polisi walimuweka chini ya ulinzi mkali mtuhumiwa huyo, waliyemkamata katika mji mdogo wa Laela akiwa na risasi 30 za bunduki aina ya AK-47 anazodaiwa kuzisafirisha mkoani Mbeya, ambako amekuwa akifanya vitendo vya ujambazi.


Alisema baada ya kuhojiwa alikiri kuwa anamiliki bunduki na polisi walimchukua akiwa chini ya ulinzi mpaka porini karibu na nyumbani kwake, ili akawaonyeshe silaha hiyo na aliwatolea bunduki ya kivita aina ya SMG yenye namba za usajili 56-3806320 ikiwa imehifadhiwa katika mifuko ya sandarusi.


Wakati polisi wakiwa wanaendelea kuiangalia silaha hiyo, ghafla mtuhumiwa alitoroka na kuanza kutimua mbio, ndipo polisi walimkimbiza bila mafanikio na kuamua kutumia silaha kumpiga risasi mgongoni, kiunoni na mguuni.


Alisema polisi walijitahidi kumuwahisha Hospitali ya Mkoa ya Sumbawanga, lakini alifariki dunia akiwa njiani.


Kamanda Kyando alisema marehemu alikuwa anasakwa kwa muda mrefu kutokana na vitendo vyake vya ujambazi na mauaji katika mikoa ya Mbeya, Songwe, Rukwa, Katavi, Tabora na Kigoma na amekuwa akitembelea maeneo hayo kwa ajili ya kufanya uhalifu wa kutumia silaha.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527