WAZIRI WA UJENZI AMUAGIZA MKANDARASI KUKAMILISHA MRADI WA BARABARA YA NYAKANAZI - KABINGO KABLA YA AGOSTI 30

Waziri wa Ujenzi ,Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isaack Kamwelwe amemuagiza mkandarasi wa mradi wa barabara ya Nyakanazi Kabingo Nyanza road work kuhakikisha ifikapo Agosti 30 mwaka huu kilometa 23 kati ya kilometa 50 za lami ziwe zimekamilika kujengwa kwa kiwango cha lami.

Waziri huyo aliyatoa maagizo hayo jana wilayani Kakonko mkoani Kigoma wakati alipoanza ziara yake akitokea mkoani Geita ambapo alianza kwa kutembelea barabara hiyo inayounganisha mkoa wa Kigoma na mikoa mingine ambapo alisema wananchi wa mkoa wa Kigoma hawajawahi kuona lami wanashauku kubwa ya kuona barabara hiyo ya lami inakamilika na Rais amewaletea mradi huo lazima na wao wafaidi ndani ya utawala wa awamu ya tano kwa kupata barabara.

Kamwele alisema barabara hiyo ilitakiwa iwe imekamilika na kumuagiza Meneja msimamizi wa mradi huo endapo atashindwa kukamilisha kilometa 23 akirudi mwezi wa nane mwishoni atarudi na tiketi yake ili aweze kurudi nchini kwao na kuwataka Kampuni ya Nyanza road work kumsimamia mtu waliyemuajiri kufanya kazi usiku na mchana ili mradi ukamilike kwa wakati.

"Leo nimeanza kumkagua Nyanza road work sijaridhishwa na mradi unavyoendelea ,mradi huu umeanza mwaka 2014 na ulitakiwa uwe umekamilika naomba nitakaporudi nipite kwenye kilomita za lami tulizokubaliana na Meneja wa mradi ambazo zimekamilika sina namna nyingine endapo hautafikia kiwango hicho nitamuomba mkandarasi alete meneja mwingine akishindwa nae tutatafuta mkandarasi mwingine, hatutajali kwamba yeye ni kampuni ya kitanzania hatuwezi kuwavumilia katika maeneo ya kucheza sio mkoa wa Kigoma wananchi wameteseka na vumbi muda mrefu", alisema mhandisi Kamwelwe.

Aidha alisema wametanganza tenda ya mradi mwingine wa Kabingo hadi Nduta ,kilomita 89 baada ya miezi miwili watasainiana mkataba na mkandarasi mwingine aanzie hapo, malengo ni miaka miwili maeneo yote yaliyobaki mkoani Kigoma yatakuwa na wakandarasi ili mkoa wa Kigoma ufunguke kwa kiwango cha lami.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Kakonko Kanali Hosea Ndagala alisema wananchi wanataka barabara iwepo na lami wamechoka vumbi kila siku, na kuwataka wakandarasi kasi walioionyesha leo baada ya kusikia waziri anakuja waendeleze kasi hiyo na yeye kama mkuu wa Wilaya atahakikisha anasimamia waweze kukamilisha kilomita hizo walizopangiwa kwa wakati.

Waziri wa ujenzi amewasili mkoani Kigoma katika ziara yake ya siku tatu ambapo atatembelea barabara za Nyakanazi Kabingo na Kasulu Kidahwe zenye wakandarasi, pamoja na kutembelea bandari ya Kigoma na uwanja wa ndege.
Na Rhoda Ezekiel - Malunde1 blog
Katikati ni Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isaack Kamwelwe kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Kakonko Kanali Hosea Ndagala  na kulia ni meneja wa mradi wa barabara ya Nyakanazi Kabingo  kutoka kampuni ya Nyanza road  work  wakipokea maelekezo ya waziri - Picha na Rhoda Ezekiel - Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527