Picha : AJALI YA BASI LA KING MSUKUMA,GARI DOGO YAUA WATU WATANO,KUJERUHI 36 GEITA


Watu watano wamefariki dunia na wengine 36 kujeruhiwa baada ya basi walilokuwa wakisafiria kutoka Mwanza kwenda Bukoba kugongana na gari ndogo aina ya Harrier ilitokea eneo la Kasamwa wilayani Geita leo Jumapili Juni 17,2018.

 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Mponjoli Mwabulambo amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo.

Mabasi ya King Msukuma yanamilikiwa na mbunge wa Geita vijijini, (CCM) Joseph Kasheku maarufu kwa jina la Msukuma.

Kaimu Mganga Mfawidhi Hospitali ya Mkoa wa Geita, Dk Mazoea Fimbo amesema maiti za watu watano, wanawake wanne na mtoto anayekadiriwa kuwa na umri wa miezi sita zimepokelewa na kuhifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti hospitalini hapo.

"Majeruhi watatu wamehamishiwa Hospitali ya Rufaa ya Bugando jijini Mwanza kwa matibabu zaidi kutokana na hali zao kuwa mbaya na kuhitaji huduma Maalum," amesema Dk Fimbo.

Akizungumzia ajali hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Geita, Robert Gabriel amesema kwa mujibu wa maelezo ya mashuhuda, ajali hiyo ilitokea baada ya basi kukosa mwelekeo na kulifuata gari dogo upande wa kulia wa barabara na kuligonga ubavuni kabla ya magari yote mawili kupinduka. 
Na Joel Maduka - Geita







Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527