PADRI ANAYEVUMA KWA RAP ' KUFOKA FOKA KANISANI' ASIMAMISHWA KAZI


Kasisi mmoja wa kanisa Katoliki nchini Kenya aliyepata umaarufu kutokana na mtindo wake wa kutumbuiza kwa kutumia muziki wa kufoka amesimamishwa kazi.


Paul Ogalo aka 'Sweet Paul' amekuwa akitumia muziki wa rap kama njia ya kuwavutia vijana wengi kufika kanisani.

Alikuwa amesema muziki ni njia mwafaka sio tu kuwavutia vijana bali pia kueneza Injili.

Mistari ya nyimbo zake huwa kwa mfano: "Kujeni church kuna baraka, kujeni church kuna baraka..." au "Father Paul, niki-lock kwenye mic, Nduru inafuata, mamanze go tipsy, vijana ruka ruka swag ya kunguru, au sio"

Lakini hatua yake hiyo inaonekana kutowafurahisha viongozi wa kanisa Katoliki magharibi mwa Kenya ambao wamemsimamisha kazi kwa mwaka mmoja ili "ajitafakari".

Askofu wa jimbo la kanisa Katoliki la Homa Bay Philip Anyolo amesema padri huyo ni lazima achague kati ya kuwa „rapa na kuwa padri".

Amesema kasisi huyo hataruhusiwa kuongoza ibada ya misa kwa kipindi cha mwaka mmoja ingawa anaruhusiwa kushiriki ibada, na pia anaruhusiwa kufanya ibada ya misa lakini faraghani.
Kasisi Ogalo amekuwa akibadilisha mavazi ya upadri baada ya misa na kuvalia fulana ndefu za rangi nyekundu au nyeusi, suruali isiyobana mwili pamoja na kujifunga kitambaa kichwani na kutumbuiza kwa nyimbo kama wafanyavyo wanamuziki wa rap.

Hilo limekuwa likiwafurahisha vijana wengi na hata waumini wengine wa umri mkubwa.

Askofu Anyolo amesema uamuzi wa kumsimamisha kazi ulifikiwa mwezi uliopita.

Hata hivyo amesema kasisi huyo yuko huru kuendelea kutumia muziki wa rap na njia nyingine za kutumbuiza kuwahubiria vijana "lakini hafai kufanya hivyo kwenye altari."

"Mambo ya kidini na mambo ya kidunia hayawezi kuchanganywa. Padri Ogallo ana kipindi cha mwaka mmoja cha kujitafakari na kuamua iwapo amejitolea kufuata maisha kamili ya upadri," amesmea askofu huyo.

Padri huyo aliambia BBC kwamba hado hajapata taarifa za kusimamishwa kazi kwake na wakuu wa kanisa, ila amekuwa akisikia tu taarifa mitandaoni.

"Niligundua ya kwamba vijana wanapenda muziki, ndio maana wanaenda maeneo ya burudani, hivyo nikasema kama wanapenda hivyo basi hiyo ndiyo nitawapatia," aliambia BBC awali.

"Mimi naimba muziki wa aina yoyote, wa injili, riddims, hip-hop, lingala, raga, reggae pamoja, ili niwape mchanganyiko kamili."

"Watu wengi hawana shida, wanaona hiyo ni talanta, lazima niiendeleze. Lakini wachache ndio wako na shida, lakini swali ni kwamba kanisa liko ndani ya ulimwengu na ulimwengu uko ndani ya kanisa, kwa hivyo hakuna tatizo mambo ya dunia na ya kanisa yanaenda sambamba, bora tu wafundishwe mambo mazuri ya maisha."

Chanzo- BBC

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527