COASTER YAGONGA MKOKOTENI TINDE,YAUA NA KUJERUHI



Mwanamke aliyejulikana kwa jina la Happiness Segesa (30-35) amefariki dunia na wengine wawili kujeruhiwa baada ya gari lenye namba za usajili T.894 Toyota Coaster kugonga mkokoteni wa kusukumwa na punda katika barabara ya Nzega kuelekea Tinde ,eneo la kijiji cha Nsalala kata ya Nsalala wilaya ya Shinyanga mkoani Shinyanga.


Inaelezwa kuwa basi dogo aina ya Coaster ligonga tela la kukokotwa na ng'ombe/punda 'mkokoteni' lililokuwa limebeba watu na wengine wakitembea kwa miguu wanadaiwa walikuwa wakitoka ngomani Nsalala - Tinde wilaya ya Shinyanga usiku huu majira ya saa mbili usiku wa Jumatano Juni 27,2018.

Mashuhuda wa tukio hilo wanasema mwanamke huyo alipoteza maisha eneo la ajali huku watu watano akiwemo mtoto anayekadiriwa kuwa na miaka minne wakijeruhiwa na kupatiwa matibabu katika kituo cha afya Tinde na wengine kukimbizwa katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Shinyanga.

"Coaster iligonga watu waliokuwa wamepanda kwenye mkokoteni na wengine wakitembea karibu na mkokoteni..walikuwa wanatoka kwenye ngoma ya asili Nsalala ambapo kulikuwa na mpambano wa ma manju wawili Madebe na Inaga",ameeleza diwani wa kata ya Tinde,Japhar Kanolo.

Kamanda wa jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga ACP Simon Haule amesema chanzo cha ajali hiyo ni mkokoteni kuingia barabara kuu bila kuchukua tahadhari na mkokoteni huo kutokuwa na viakisi mwanga.

Amesema majeruhi wawili Alice Malunde (25) aliyevunjika mguu wa kulia na Juma Ndegesela (34) aliyepata michubuko sehemu mbalimbali za mwili wake wamelazwa katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Shinyanga.

Na Kadama Malunde - Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527