MWILI WA MWANDISHI WA HABARI MWALIMU STEPHEN KIDOYAYI,KUAGWA SHINYANGA..KUZIKWA BARIADI

Mwili wa mwandishi wa habari marehemu Stephen Peter Kidoyayi utaagwa kesho Ijumaa,Mei 18,2018 asubuhi Mjini Shinyanga kisha kusafirishwa kwenda katika kijiji Itubukilo wilayani Bariadi mkoani Simiyu kwa ajili ya mazishi.

Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa Klabu ya waandishi wa habari mkoa wa Shinyanga,bwana Kadama Malunde,mwili wa Stephen Kidoyayi upo nyumbani kwake katika shule ya Sekondari Buhangija mjini Shinyanga,shule ambayo amekuwa akifundisha kwa muda mrefu. 

"Mbali na kuwa mwandishi wa habari,Kidoyayi pia alikuwa mwalimu katika shule ya Sekondari Buhangija,Shughuli za kuaga mwili zitaanza saa moja asubuhi shuleni kisha nyumbani kwake,baada ya hapo safari ya kusafirisha mwili wa marehemu kwenda Bariadi mkoani Simiyu itaanza,mazishi yanatajiwa kufanyika kesho Ijumaa",ameeleza Malunde.

Kidoyayi ambaye alikuwa anaandikia gazeti la Jamboleo kabla ya kuhamia gazeti la Tanzanite hivi karibuni na pia alikuwa mwalimu wa Buhangija Sekondari amefariki dunia jana Jumatano wakati akipatiwa matibabu katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Shinyanga baada ya kuugua kwa muda mfupi.

Kidoyayi alizaliwa mwaka 1964 mbali na kuwa mwalimu pia amewahi kuandikia magazeti mbalimbali ikiwemo Msanii Afrika,Shaba,Nyundo,Jamboleo na Radio Free Africa.

 Pia ni miongoni mwa waanzilishi wa Klabu ya waandishi wa habari mkoa wa Shinyanga iliyoanzishwa mwaka 2003.
Amewahi kuwa mweka hazina wa klabu ya waandishi wahabari mkoa wa Shinyanga (2004 -2007),Katibu Mtendaji (2007 - 2010) na Mjumbe wa kamati tendaji ya klabu hiyo tangu mwaka 2010 hadi umauti unamkuta.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527