RAIS MAGUFULI ACHEKELA UKIMYA WA MIZENGO PINDA....AMMWAGIA SIFA KEM KEM

Rais John Magufuli jana alimmwagia sifa Waziri Mkuu mstaafu, Mizengo Pinda kwa kumwelezea ni kiongozi mkimya na asiyependa kuzungumza ovyo ovyo.


Rais Magufuli alisema Pinda, maarufu kama Mtoto wa Mkulima, ni kiongozi anayefaa kuigwa na viongozi wengine, na kwamba hata yeye siku akistaafu atamfuata ili kujifunza.


Aliyasema hayo jana mjini Dodoma wakati akifungua Tawi la Benki ya NMB la Kambarage na Jengo la Mfuko wa Pensheni kwa Watumishi wa Umma (PSPF).


“Mzee Pinda anaishi maisha ya kawaida sana, hapigi kelele, hazungumzi chochote, Mzee Pinda ‘you are too special’ (wewe ni mtu wa kipekee),” alisema Rais Magufuli.


“Watu watakukumbuka (Pinda) kwa ukarimu wako, wewe ni mtu wa kawaida sana. Sasa hivi hatujui thamani yako lakini ipo siku tutaijua.


“Ndiyo maana bado unaonekana kijana, hujipi ‘pressure’ (hofu), unaamini kile unachofanya, na mimi nikistaafu nitakuja kuchukua ‘course’ (mafunzo) kwako.”


Sifa kwa Pinda zinakuja miezi saba tangu alipokosoa viongozi wastaafu wa "maeneo mengine" wanaosemasema kila wakati kuhusu uendeshaji wa serikali.


Akizungumza jijini Dar es Salaam Septemba 11, mwaka jana Rais Magufuli alitoa mfano wa majaji wastaafu ambao alisema ni tofauti na wastaafu wengine na kwamba huenda kujua sheria ndiko kunakowasaidia kutokuwa waropokaji.


Rais Magufuli alisema hayo wakati wa kumuapisha Jaji Mkuu Profesa Ibrahim Juma.


“Nawashuruku majaji wakuu wastaafu, Barnabas Samatta na Augustino Ramadhani, walifanya kazi kubwa ya kujenga misingi ya mahakama nchini," alisema.


“Bahati nzuri majaji hawa ni waadilifu sana huwezi kumsikia Jaji (Mkuu mstaafu Othman) Chande, (Barnabas) Samatta, Augustino (Ramadhani), (Damian) Lubuva au majaji walioko hapa... ukiangalia wastaafu wa maeneo mengine hawachoki kusema, wanawashwawashwa.


“Ndiyo maana nawapongeza sana mahakama...Ni safi mno, nina uhakika wanapotaka kutoa ‘advice’ (ushauri) yoyote (wowote) lazima wanakushirikisha (Jaji Mkuu); ndiyo faida ya kujua sheria.


“Sisi wengine huku ambao hatujajua sheria mahali popote, chochote unaweza ukazungumza.”

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527