KAULI YA RAIS MAGUFULI AKISHIRIKI MAADHIMISHO YA MISA TAKATIFU YA PASAKA KANISA LA MT. JOSEPH DAR

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli tarehe 01 Aprili, 2018 ameungana na Wakristo wote Tanzania katika maadhimisho ya Misa Takatifu ya sikukuu ya Pasaka iliyofanyika katika Kanisa la Mtakatifu Joseph, Jimbo Kuu la Dar es Salaam.

Misa hiyo imeongozwa na Paroko Msaidizi wa Parokia ya Mtakatifu Joseph Padre Venance Tegete.

Akizungumza baada ya kukaribishwa na Padre Tegete kutoa salamu, Mhe. Rais Magufuli amewatakia Watanzania wote heri ya Pasaka na ametoa wito kwa Watanzania kuendelea kuishi kwa amani na upendo huku wakishiriki ipasavyo katika ujenzi wa Taifa.

“Kifo na ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo ukafufue matendo yetu, tuendelee kuijenga amani yetu, upendo wetu na tujenge maendeleo ya Watanzania wote, kwani Kristo alifundisha upendo miongoni mwetu.

“Kwa hiyo Baba nakushukuru sana kwa kuongoza Misa hii, naomba ufikishe shukrani zangu kwa Kardinali Pengo, Maaskofu wote na Watanzania wote tuendelee kusimama pamoja ili kulijenga Taifa letu” amesema Mhe. Rais Magufuli.

Mhe. Rais Magufuli aliongozana na Mkewe Mhe. Mama Janeth Magufuli.

Gerson Msigwa

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU.

Dar es Salaam

01 Aprili, 2018



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527