DEGE LA EMIRATES LILILOBEBA ABIRIA 475 LATUA KWA DHARURA DAR


Ndege kubwa ya kampuni ya Emirates 'Dege' iliyokuwa ikielekea Mauritius ikiwa na abiria 475 wakitokea Dubai, imetua jijini Dar es Salaam jana kwa dharura kutokana na hali mbaya ya hewa nchini humo.


Kamanda wa Polisi wa Viwanja vya Ndege Tanzania, Kamishna msaidizi, Matanga Mbushi amethibitishia taarifa hizo akisema ndege hiyo ya Emirates, aina ya Airbus 380, EK701, ilishindwa kutua mara tatu nchini Mauritius kutokana na mvua kali iliyokuwa ikinyesha.

“Hiyo ndege ilikuwa ikielekea Mauritius, sasa hali ya hewa imekuwa mbaya ikashindwa kutua. Rubani alijaribu kutua mara tatu lakini akashindwa ndipo akaamua kuja Dar es Salaam kutua kwa dharura,” alisema Mbushi.

Amesema ndege hiyo ilikuwa na abiria 475 na wote wamepangiwa hoteli ili kusubiri taarifa za hali ya hewa ikiwa nzuri waendelee na safari.


“Kesho kama hali itakuwa nzuri wataondoka,” amesema Mbushi.


Ndege hiyo ni ya Shirika la Emirates la Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE). Ni kampuni tanzu ya Emirates Group, ambayo inamilikiwa na Shirika la Uwekezaji la Serikali ya Dubai.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527