WANAKIJIJI WAPIGWA MARUFUKU KUOA WALA KUOZESHA BILA KUJISALIMISHA SERIKALI YA KIJIJI SHINYANGA

Mwenyekiti wa kijiji cha Nsalala Sandeko Ndegeleja Machungo

Serikali ya kijiji cha Nsalala kata ya Nsalala Tarafa ya Itwangi halmashauri ya wilaya ya Shinyanga imetunga sheria ya kutokomeza ndoa za utotoni kwa kupiga marufuku kila mwananchi anayetaka kuoa ama kuozesha lazima atoe taarifa kwa uongozi wa kijiji hicho.

Sheria hiyo inamtaka kila mwananchi kutoa taarifa kwa uongozi wa kijiji ndiyo apatiwe ridhaa ya kufunga pingu za maisha. 



Hayo yamesemwa leo Ijumaa Machi 30,2018  na mwenyekiti wa kijiji cha Nsalala Sandeko Ndegeleja Machungo wakati wa mdahalo kuhusu Ukatili wa Kijinsia  ulioandaliwa na Shirika la Kivulini kwa ufadhili wa shirika la Oxfam  


Alisema viongozi wa serikali hiyo ya kijiji mara baada ya kupata elimu ya ukatili wa kijinsia kupitia mashirika mbalimbali,likiwemo shirika la Kivulini waliona ni vyema wakatunga sheria ndogo katika kijiji hicho ya kuzuia wananchi kuoa ama kuozesha  bila ya kutoa taarifa kwenye uongozi wa kijiji.

"Ili kutokomeza ndoa za utotoni,sisi tumetunga sheria za kuhakikisha watoto hawaolewi,hivyo ukitaka kuozesha lazima utoe taarifa kisha tunajirdhisha kama huyo anayeolewa au kuoa anastahili,kama yuko chini ya umri wa miaka 18 basi tunachukua hatua",alisema Ndegeleja.

Alisema kijiji kilikubaliana kutunga sheria hiyo mwaka jana na wananchi wamekuwa wakifanya hivyo na tangu ianze kufanya kazi hakuna changamoto tena ya ndoa kwa watoto wala mimba kwa wanafunzi.

Kaimu Ofisa Ustawi wa Jamii halmashauri ya Shinyanga Aisha Omari aliipongeza serikali ya kijiji hicho na kutoa wito kwa vijiji vingine kuiga kwani mapambano dhidi ya mimba na ndoa za utotoni yanahitaji nguvu ya pamoja.

Na Kadama Malunde - Malunde1 blog


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527