TUNDU LISSU KUREJEA NCHINI BAADA YA KUFANYIWA UPASUAJI WA MGUU?


Alute Mughwai, kaka wa mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu amesema ndugu yake atakaa kwa wiki mbili katika hospitali ya Leuven Gasthuisberg ya nchini Ubelgiji baada ya kufanyiwa upasuaji wa mguu wake wa kulia.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Machi 15, 2018 Mughwai amesema kutokana na operesheni hiyo, Lissu ambaye alikuwa akipatiwa matibabu hospitali na kurejea kwenye makazi yake, sasa atakaa hospitali kati ya siku saba hadi 10.


Amesema upasuaji katika mguu huo, ambao awali ulionekana kutounga vizuri, ulikwenda vizuri na madaktari wa hospitali hiyo wamemtaka alazwe ili kupata matibabu zaidi.

Wakili Mughwai ambaye ndiye msemaji wa familia ya Lissu, amesema baada ya siku 10, Madaktari watatoa taarifa juu ya maendeleo ya afya yake na mazoezi ya viungo ambayo alikuwa anaendelea nayo.

"Kutokana na maelekezo ya madaktari kwa sasa, hatuwezi kusema Lissu atarudi lini nchini, kwani upasuaji wa jana umesababisha alazwe tena hospitali"alisema.

Amewaomba Watanzania na watu wengine, kuendelea kumuombea Lissu ili apone haraka na arejee nchini.

Akizungumzia matibabu ya Lissu, amesema wanaomba watanzania na wasamaria wema, kuendelea kumchangia Lissu kupitia akaunti iliyotolewa na Chadema.

“Bado tunafanya mazungumzo kujua kama itawezekana awe na akauti nyingine Ubelgiji ili kusaidia matibabu kwani hadi sasa anatibiwa kwa misaada wa watanzania na watu wengine kutoka nje ya Tanzania,” amesema

Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu ambaye ni rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) jana Machi 14, 2018 alifanyiwa upasuaji wa mguu wa kulia kama alivyoshauriwa na madaktari wa Hospitali ya Chuo Kikuu cha Leuven, Gasthuisberg nchini Ubelgiji.

Lissu amesema operesheni hiyo iliyochukua saa mbili ilifanywa na timu ya madaktari bingwa chini ya uongozi wa Profesa Willem-Jan Mertsemakers.

“Operesheni ilienda vizuri na kwa sasa naendelea na dawa na mapumziko hospitalini kwa muda wa angalau wiki tatu zinazokuja,” amesema Lissu.

“Wameniwekea chuma cha kuimarisha mfupa wote wa paja la kulia. Pia wamechukua vipimo ili kuangalia kama hakuna tatizo la bacteria kabla hawajafunga kabisa sehemu ya kwenye goti ambayo haijaunga hadi sasa.”

Mke wa Lissu, Alicia amesema anamshukuru Mungu kwamba upasuaji huo umekwenda vyema.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527