JINSI MWILI WA MMILIKI WA MABASI YA SUPER SAMI ULIVYOKUTWA KWENYE KIROBA MTONI




Jeshi la Polisi mkoa wa Kipolisi Mara, limetoa taarifa rasmi juu ya kuokotwa kwa mwili wa mfanyabiashara na mmiliki wa mabasi ya Super Sami Samson Josiah , ambaye alitoweka na mwili wake kuokotwa mtoni hapo jana.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Mara Jafari Mohamed, amesema hapo jana walipata taarifa kutoka kwa wananchi kuhusu kuokotwa kwa kiroba chenye mwili ndani, na walipokifungua na kuita watu kutambua, ndipo alipojulikana kuwa ni mwili wa mfanya biashara huyo anayeishi mkoani Mwanza.

“Jana jioni tumeweza kupata mwili wa marehemu huyu Samson Josiah ambaye ni mmiliki wa mabasi ya Super Sammy anayeishi Mwanza, kwamba kuna mwili umeonekana katika mto ambao unatenganisha mkoa wa Mara na mkoa wa Simiyu unaoelekea mbugani Serengeti, wananchi waliona kiroba kimefungwa kinaelea, kikavutwa wakajulishwa polisi kufungua ndani wakakuta mwili wa marehemu, kwa sababu tulikuwa na taarifa za utafutaji na mashaka juu ya kutoweka kwake, tukajulisha ndugu hao na wakatambua mwili wa marehemu”, amesema Kamanda Mohamed.

Kamanda Mohamed aliendelea kwa kueleza kwamba marehemu alitoweka kuanzia tarehe 27 mwezi wa pili ambapo aliondoka mkoani Mwanza, na ndugu zake walisema kuwa aliaga anaenda Simiyu kwa shughuli zake za kibiashara na kuna mtu anamdai na akapotea tangu siku hiyo, na gari yake aliyotoka nayo Mwanza kukutwa imechomwa moto maeneo ya Serengeti mnamo tarehe 8 hadi kuteketea kabisa.

Imeelezwa kwamba kwa sasa mwili huo umehifadhiwa hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Mara kwa ajili ya postmoterm, na baadaye utatolewa kwenda kuzikwa.

Mpaka sasa watu wanne wameshikiliwa kufuatia tukio hilo, upelelezi bado unaendelea.
Chanzo- EATV

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527