MTUHUMIWA WA MAANDAMANO CHADEMA ADAI GARI LAKE POLISI

Mfuasi wa CHADEMA, Ally Rajabu anayekabiliwa na kesi ya kufanya mkusanyiko usio halali ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa anaomba arejeshewe gari lake ambalo lipo mikononi mwa polisi.


Ally Rajabu ni mshtakiwa wa 28 kati ya 31 wakiwemo watatu waliopigwa risasi na Polisi ambao ni wafuasi wa chama hicho wanaokabiliwa na kesi ya kufanya mkusanyiko usio halali maeneo ya Kinondoni Mkwajuni Dar es Salaam.


Awali kabla ya kueleza hayo, Wakili wa Serikali Aldo Mkini, amemueleza Hakimu Mkazi Mkuu, Wilbard Mashauri kuwa upelelezi wa shauri hilo bado haujakamilika.


Naye Wakili wa utetezi, Alex Massaba amedai kuwa wateja wake wawili ni wagonjwa na wameshindwa kufika mahakamani hapo.


Baada ya kueleza hayo, mshtakiwa wa 28, Ally Rajabu ameieleza mahakama kuwa anaomba kurudishiwa gari lake ambalo linashikiriwa na Jeshi la Polisi tangu siku ya maandamano.


Hata hivyo, Hakimu Mashauri amesema kuwa mahakama hiyo haina uwezo wa kuingilia masuala yaliyofanyika Polisi ambapo ameahirisha kesi hiyo hadi April 4, 2018.


Washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni Thabitha Mkude, Khaji Lukwambe, Emmanuel Kimio, Mohamed Juma, Husein Mnimbo na wenzao kwa pamoja wanadaiwa kati ya February 16, 2018 maeneo ya Mkwajuni Kinondoni DSM walifanya mkusanyiko usio wa halali kinyume cha sheria.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527