MWANASIASA WA UPINZANI ALIYEIDHINISHA KIAPO CHA ODINGA AFUKUZWA TENA KENYA,ARUDISHWA DUBAI

Bw Miguna amesambaza picha anazosema ni zake akiwa hospitalini kumuona daktari uwanja wa ndege Dubai

Mwanasiasa wa upinzani Kenya aliyeidhinisha kiapo cha kiongozi wa upinzani Raila Odinga kuwa 'Rais wa Wananchi' Januari Miguna Miguna ametimuliwa tena kutoka nchini humo.

Mwanasiasa huyo ametimuliwa huku mzozo kuhusu uraia wake ukiendelea.

Mashirika ya kutetea haki za kibinadamu, Tume ya Taifa ya Haki za Kibinadamu Kenya (KNCHR) na shirika la kimataifa la Human Rights Watch wameishutumu hatua ya serikali ya kuendelea kumzuia Bw Miguna kurejea Kenya.

Bw Miguna asubuhi aliandika kwenye Facebook kwamba aliamka na kujipata yuko Dubai na kwamba anahitaji matibabu.

Alisema anafahamu kwamba kuna mpango wa kumpeleka London lakini alitaka kupanda ndege ya kurejea Nairobi pekee.

Mwanasiasa huyo alisema alisindikizwa na afisa wa idara ya ujasusi na kwamba amemuona daktari uwanja wa ndege.

Bw Miguna alisisitiza kwamba hatasafiri kwenda popote ila kurejea Nairobi.

Serikali imechukua hatua hiyo licha ya kuwepo kwa maagizo ya mahakama ya kuzuia kutimuliwa kwake na ya kuitaka serikali kufanikisha kurejea kwake nchini humo.

Bw Miguna alikuwa amezuiliwa uwanja wa ndege wa kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA) tangu alipowasili Jumatatu adhuhuri.

Mwanasiasa huyo alikuwa anajaribu kurejea kutoka Canada ambako alikuwa amepelekwa baada ya kufurushwa kutoka Kenya kwa lazima mwezi Februari.

Jaji wa Mahakama Kuu George Odunga Jumatano alisema waziri wa usalama nchini humo, mkuu wa polisi na mkuu wa idara ya uhamiaji watakuwa wamekaidi maagizo ya mahakama iwapo wangekataa kumwachilia huru.

Alikuwa ametoa ilani kwa watatu hao kufika mahakamani baadaye Jumatano lakini baada yao kukosa kufika akawapata na hatia ya kukaidi agizo la mahakama.

Aliahidi kutoa adhabu dhidi yao leo asubuhi lakini kikao kilipoandaliwa akatoa muda kwa mawakili wa serikali kujaribu kuona iwapo maafisa hao watatii agizo la mahakama kabla ya kuwaadhibu.

Maafisa wa Kenya mnamo 6 Febuari walikuwa wamemfukuza kutoka nchini humo kutokana na mchango wake wakati wa kuapishwa kwa Bw Odinga.

Walisema mwanasiasa huyo hana uraia wa Kenya lakini ana uraia wa Canada.

Idara ya uhamiaji ya Kenya imekariri kuwa Miguna alipoteza uraia wa Kenya mwaka 1998 alipopewa uraia wa Canada wakati ilipokuwa ni kinyume cha sheria kuwa na uraia wa nchi mbili nchini Kenya.

Kuzuiliwa kwa Bw Miguna kumejadiliwa pakubwa kwenye mitandao ya kijamii Kenya, baadhi wakiunga mkono hatua hiyo lakini wengine wakiwashutumu maafisa wa uwanja wa ndege na serikali.

Mmoja wa mawakili wa Bw Miguna, Nelson Havi, ni miongoni mwa waliokuwa wa kwanza kufichua kwamba Bw Miguna alikuwa ametimuliwa tena nje ya nchi hiyo.
Mawakili kushambuliwa

Usiku wa kuamkia Jumanne, kabla ya kusafirishwa kwa Miguna kwenda Dubai, mawakili James Orengo, Julie Soweto, Nelson Havi na Cliff Ombeta walikuwa wamefika uwanja wa ndege wa JKIA kujaribu kuwasilisha ilani ya mahakama ya kuwataka maafisa wa uhamiaji kutomsafirisha nje ya nchi Bw Miguna.

Lakini taarifa za vyombo vya habari zinasema walishambuliwa na kupigwa na maafisa wa usalama katika uwanja huo.

Wanahabari hawajaruhusiwa pia kuingia tena uwanja huo. Baadhi walidaiwa kupigwa na kuumizwa na maafisa wa polisi wakati wa jaribio la kwanza la kumsafirisha Bw Miguna kwenda Dubai usiku wa kuamkia Jumanne.

Jumanne Roselyn Aburili alikuwa ametoa agizo Bw Miguna aachiliwe huru. Mawakili Orengo na Otiende Amollo walibandika agizo la mahakama katika milango ya afisi za uhamiaji JKIA na makao makuu ya polisi.

Baadaye Bw Havi alijaribu kuwapasha habari maafisa hao kupitia mtandao wa Twitter hatua ambayo haikupokelewa vyema na msemaji wa Wizara ya Mambo ya Ndani Mwenda Njoka.

Bw Njoka alisema hawawezi kupokea ilani ya mahakama kupitia mitandao ya kijamii.
Kukamatwa kwa Miguna mara ya kwanza

Bw Miguna alikamatwa na polisi kwa mchango wake katika kuapishwa kwa Bw Odinga kuwa "Rais wa Wananchi", hafla iliyofanyika uwanja wa Uhuru Park, Nairobi mnamo 30 Januari.

Bw Miguna, ambaye pia ni wakili, ndiye aliyetia saini hati ya kiapo ya Bw Odinga.

Serikali ilikuwa imeeleza hatua hiyo ya kiongozi huyo wa upinzani kuwa uhaini wa hali ya juu.

Bw Odinga anadai kwamba alimshinda Rais Uhuru Kenyatta katika uchaguzi mkuu wa 8 Agosti ambao matokeo yake yalifutiliwa mbali na Mahakama ya Juu kwa sababu ya kutokea kwa kasoro nyingi.

Mahakama iliamuru uchaguzi mpya ufanyike lakini Bw Odinga akasusia uchaguzi huo mnamo 26 Oktoba na kutangaza kwamba hakumtambua Bw Kenyatta kama rais halali wa nchi hiyo.

Baadaye aliongoza hafla ya kuapishwa kwake mnamo tarehe 30 Januari.

Mapema mwezi huu, Bw Odinga na Rais Uhuru Kenyatta walikutana katika mkutano ambao haukuwa umetarajiwa na wakahutubia wananchi moja kwa moja kupitia vyombo vya habari.

Waliahidi maridhiano na pia wakaahidi kuwaunganisha tena Wakenya.

Bw Miguna mnamo Jumatano alikuwa ameandika kwenye ukurasa wake wa Facebook Jumanne kwamba alikuwa anazuiliwa chooni uwanja wa ndege na kwamba alikuwa amezuiwa kuwaona mawakili wake na jamaa zake.
Miguna alipoteza uraia wake?

Chini ya Kifungu 17 cha Katiba ya Kenya, mtu aliyezaliwa nchini Kenya anaweza tu kuupoteza uraia wake iwapo itabainika kwamba aliupata uraia huo kwa njia ya ulaghai, au ibainike kwamba mtu huyo au wazazi wake walikuwa raia wa nchi nyingine, au ibainike kwamba mtu huyo alikuwa na umri wa zaidi ya miaka minane alipogunduliwa akiishi Kenya.

Serikali ya Kenya imekuwa ikisisitiza kwamba chini ya katiba ya zamani, Wakenya hawangekuwa na uraia wa nchi mbili.

Serikali inasema hatua ya Bw Miguna ya kupata pasipoti ya Canada mwaka 1988 ina maana kwamba aliupoteza uraia wa Kenya wakati huo.

Ingawa Bw Miguna aliwasilisha maombi na akapewa pasipoti ya Kenya mwaka 2009, serikali inasema pasipoti hiyo ya Kenya si halali kwa sababu hakufichua kwamba wakati huo alikuwa raia wa Canada pia.

Serikali imesema mwanasiasa huyo hakuwasilisha tena ombi la kuruhusiwa kuwa raia wa Kenya katiba ilipofanyiwa marekebisho mwaka 2010 na Wakenya wakakubaliwa kuwa na uraia wa nchi mbili.

Bw Miguna amekuwa akisisitiza kwamba hakuwahi kuukana uraia wake wa Kenya na kamwe hawezi kufanya hivyo.

"Katiba iko wazi kabisa: hakuna mtu yeytoe anayeweza au anayeweza kudai kuufuta uraia wa Mkenya aliyezaliwa nchini Kenya," alisema awali.
Matukio makuu mzozo kuhusu Miguna

30 Januari: Miguna aidhinisha hati ya kiapo cha Raila Odinga kuwa 'Rais wa Wananchi'

2 Februari: Atangaza kwamba amekamatwa na polisi Nairobi

6 Februari: Afurushwa kutoka Kenya na kupelekwa Canada

16 Machi: Odinga waambia wafuasi wake kwamba baada ya mapato yake na Bw Kenyatta, Miguna anafaa kuruhusiwa kurejea Kenya bila masharti

26 Machi: Arejea Kenya lakini azuiliwa uwanja wa ndege wa JKIA. Baadaye usiku, anusurika jaribio la kumpeleka Dubai.

28 Machi: Miguna apelekwa Dubai kwa nguvu. Asema anafahamu mipango ya kumpeleka hadi London.
Miguna Miguna ni nani?

Miguna alizaliwa katika kijiji cha Magina, katika jimbo la Kisumu, magharibi mwa Kenya.

Bw Miguna amekuwa kiongozi wa kundi linaloitwa National Resistance Movement (NRM, Vuguvugu la Taifa la Kupinga Serikali), ambalo liliundwa na muungano wa upinzani wa National Super Alliance siku moja kabla ya kufanyika kwa uchaguzi wa marudio ambao Bw Odinga alisusia mnamo 26 Oktoba mwaka jana.

"Utakuwa ni muungano wa ukombozi," alisema Bw Odinga akitangaza kuundwa kwa vuguvugu hilo.

"Tumesema hatutaheshimu serikali dhalimu."

Bw Miguna baadaye alijitangaza kuwa Jenerali wa NRM.

Mnamo 30 Januari, siku ya kuapishwa kwa Bw Odinga kuwa 'Rais wa Wananchi', muungano huo uliorodheshwa kuwa kundi haramu na waziri wa usalama Dkt Fred Matiang'i.

Hiyo haikuwa mara ya kwanza kwa Bw Miguna kujipata akikabiliana na serikali na nguvu zake.

Mwaka 1988, alikamatwa na serikali ya wakati huo ya Rais Daniel arap Moi.

Bw Miguna baadaye alitorokea Kenya ambapo alipata hifadhi kama mkimbizi wa kisiasa.

Alirejea nchini Kenya na akashiriki katika kampeni za uchaguzi za Bw Odinga na chama chake cha Orange Democratic Movement (ODM) mwaka 2007.

Uchaguzi wa mwaka huo ulikumbwa na utata na baada ya serikali ya muungano kati ya Bw Odinga na Rais Mwai Kibaki kuundwa, ambapo Bw Odinga aliteuliwa kuwa Waziri Mkuu, Bw Miguna alihudumu kama mmoja wa washauri wake kati ya 2009 na 2011

Wawili hao walizozana na Bw Miguna akawa mmoja wa wakosoaji wakuu wa Bw Odinga.

Aliandika kitabu kwa jina Peeling Back the Mask ambapo alimkosoa sana Bw Odinga na uongozi wake.

Mwaka 2013, alimuunga mkono Bw Kenyatta katika uchaguzi wa urais mwaka huo.

Lakini alibadilisha tena msimamo wake na kurejea upande wa Bw Odinga mwaka 2017, mwaka ambao aliwania pia wadhifa wa Gavana wa Nairobi katika uchaguzi uliofanyika Agosti ingawa kama mgombea ambaye hakuwa na chama.

Januari 30 mwaka huu, ndiye aliyetia saini hati ya kiapo cha Bw Odinga kuwa 'Rais wa Wananchi'.

Bw Odinga alipokutana na Bw Kenyatta mnamo 9 Machi na wakaahidi kuunganisha Kenya, Bw Miguna ni miongoni mwa waliomkosoa kiongozi huyo wa upinzani kwa hatua hiyo akisema huo ulikuwa sawa na usaliti.

CHANZO- BBC

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527