BASI LAZAMA KWENYE MTO WENYE VIBOKO SERENGETI


Basi la kampuni ya Kimotco lililokuwa linatoka Musoma, kwenda Arusha, kupitia Mugumu, limezama katika mto wenye viboko ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti mkoani Mara.


Mhifadhi mkuu wa Hifadhi hiyo William Mwakilema amethibitisha kupata taarifa ya tukio hilo leo Machi 16,2018.


Mwakilema amesema hakuna majeruhi wala vifo na kuwa abiria wote wako juu ya basi.

“Jitihada za kuwaokoa mmoja mmoja zinaendelea. Baada ya kusombwa na maji abiria wote wako juu ya basi maana halikuzama lote, jitihada za kuwaokoa zinaendelea mpaka sasa zaidi ya abiria wanne wametolewa,"amesema bila kutaja idadi ya abiria wote.

Kamanda wa Polisi mkoa Mara, Jafari Mohamed hakuweza kupatikana kwa njia ya simu, hata hivyo polisi wilayani Serengeti wamesema wameshatoa taarifa kituo kidogo cha cha polisi Seronera kufuatilia.


Mmoja wa mawakala wa kampuni hiyo Neema Kegocha amekiri kupata taarifa na kudai wanatafuta usafiri wa kwenda eneo la tukio.

Na Anthony Mayunga, Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527