AGPAHI YAKUTANA NA WADAU WA VVU NA UKIMWI MKOA WA MWANZA

Shirika la Ariel Glaser Pediatric AIDS Healthcare Initiative (AGPAHI) limeendesha kikao cha wadau wanaohusika katika mapambano ya VVU na Ukimwi mkoani Mwanza kwa ajili ya kujadili na kupanga mikakati ya kupambana na Virusi Vya Ukimwi (VVU) na Ukimwi mkoani humo.

Kikao hicho cha siku mbili kilichoandaliwa na shirika la AGPAHI kwa ufadhili wa Watu wa Marekani kupitia Centres for Disease Control (CDC), kimefanyika Machi 27,2018 hadi Machi 28,2018 katika ukumbi wa Gold Crest jijini Mwanza.

Miongoni mwa wadau waliohudhuria kikao hicho ni waratibu wa Ukimwi ngazi ya mkoa na wilaya,wakuu wa wilaya,wakurugenzi wa halmashauri,waganga wakuu wa wilaya,waratibu wa afya ya uzazi na mtoto,waratibu wa kifua kikuu,mashirika,taasisi na wadau mbalimbali wanaofanya shughuli za kupambana na VVU na Ukimwi.

Akifungua kikao hicho,Mkuu wa mkoa wa Mwanza,John Mongella alisema mapambano dhidi ya VVU na Ukimwi yatafanikiwa tu endapo kila mdau atashiriki 

“Sisi kama mkoa wa Mwanza ni wa pili kwa idadi kubwa ya watu baada ya Dar es salaam,lakini pia tupo wa pili kwa shughuli za uchumi, takwimu za mwaka 2011/2012 zinaonesha kuwa tulikuwa na maambukizi ya asilimia 4.2 lakini mwaka 2016/2017 maambukizi yamepanda hadi kufikia asilimia 7.2”,alieleza.

“Ili tushushe asilimia hizi kubwa za maambukizi lazima wadau wote tushirikiane katika mapambano dhidi ya Ukimwi kwa kuelekeza nguvu zaidi katika kundi la vijana ambalo linapata maambukizi ya VVU kwa kasi”,aliongeza Mongella.

Aidha alisema teknolojia na utandawazi inachangia kwa kiasi kikubwa kuongezeka kwa maambukizi kwani vijana wanatumia vibaya mitandao ya mawasiliano na kusababisha kujiingiza katika tabia hatarishi zinazochongia kuwepo kwa maambukizi.

Mkuu huyo wa mkoa aliwataka wadau wa afya mkoani humo likiwemo shirika la AGPAHI ambalo limekuwa msaada mkubwa katika sekta ya afya nchini,kuendelea kushirikiana na serikali katika mapambano dhidi ya VVU na Ukimwi. 

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa shirika la AGPAHI, Dk. Sekela Mwakyusa alisema mkoa huo una takribani watu 90,000 wanaokisiwa kuwa na maambukizi ya VVU na bado hawajafikiwa.

Aliongeza kuwa shirika hilo lina mpango wa kuwafikia watu wapatao 37,900 kwa ajili ya kuwapatia huduma za tiba na matunzo watu wanaoishi na maambukizi ya VVU na Ukimwi (kutokana na takwimu za utafiti wa Tanzania HIV Impact Survey (THIS) 2016 – 2017).

ANGALIA PICHA WAKATI WA KIKAO
Mkuu wa mkoa wa Mwanza,John Mongella akizungumza katika kikao cha wadau wa mapambano dhidi ya VVU na Ukimwi mkoa wa Shinyanga. Kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa shirika la AGPAHI, Dk. Sekela Mwakyusa. Kushoto ni Kaimu Mganga mkuu mkoa wa Mwanza Dk. Sylas Wambura. Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog
Mkuu wa mkoa wa Mwanza,John Mongella akiwasisitiza wadau wa afya kuungana katika mapambano dhidi ya VVU na Ukimwi.

Mkuu wa mkoa wa Mwanza,John Mongella akilishukuru shirika la AGPAHI na Watu wa Marekani kupitia CDC kwa kuendelea kushirikiana na serikali ya Tanzania katika mapambano dhidi ya VVU na Ukimwi.
Kaimu Mganga mkuu mkoa wa Mwanza Dk. Sylas Wambura akizungumza wakati wa kikao hicho. Kushoto ni Mkuu wa wilaya ya Nyamagana, Mary Tesha.
Wakuu wa wilaya na wakurugenzi wa halmashauri za wilaya mkoa wa Mwanza wakiwa ukumbini.
Mkurugenzi Mtendaji wa shirika la AGPAHI, Dk. Sekela Mwakyusa akizungumza wakati wa kikao hicho na kueleza kuwa shirika hilo litaendelea kutoa huduma za tiba na matunzo kwa watu wanaoishi na maambukizi ya VVU.
Mwakilishi wa Centres for Disease Control (CDC) nchini, Eva Matiko akizungumza katika kikao hicho.

Wadau wa masuala ya VVU na Ukimwi wakifuatilia kilichokuwa kinaendelea wakati wa kikao hicho.
Wadau wakiwa ukumbini.
Wafanyakazi wa shirika la AGPAHI mkoa wa Mwanza wakiwa ukumbini.
Mratibu wa Ukimwi mkoa wa Mwanza, Dk. Pius Masele akizungumza katika kikao hicho.
Mkuu wa wilaya ya Magu, Hadija Nyembu akichangia hoja wakati wa kikao hicho kuhusu namna ya kupambana na maambukizi ya VVU.
Mratibu wa Ukimwi,Kifua Kikuu na Malaria kutoka TAMISEMI, Mbuuni akichangia hoja wakati wa kikao hicho.
Kikao kinaendelea...



Wadau wakiwa ukumbini.

Picha zote  na Kadama Malunde - Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527