WALIOJERUHIWA KWA RISASI MAANDAMANO YA CHADEMA DAR WAACHIWA KWA DHAMANA


Watu watatu wanaodaiwa kuwa wafuasi Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, wakikabiliwa na shtaka la kufanya mkusanyiko isivyo halali.


Hata hivyo, watu hao watatu wameunganishwa katika kesi ya wafuasi 28 wa CHADEMA ambao walifikishwa mahakamani hapo wiki iliyipita.


Washtakiwa hao watatu walisomewa kosa lao mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi, Godfrey Mwambapa na Wakili wa Serikali, Patrick Mwita.


Wakili Mwita aliwataja washtakiwa hao watatu kuwa ni Isack Ng’aga, Erick John na Aida Olomi.


Wakili Mwita amedai washtakiwa hao, March 8, 2018 wataunganishwa na wenzao 28, ambao walifikishwa mahakamani hapo wiki iliyopita.


Kwa pamoja wanadaiwa kuwa February 16, 2018 huko Kinondoni katika eneo la Mkwajuni lililopo katika Wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam, walifanya mkusanyiko usio wa Halali kinyume cha sheria.


Inadaiwa kuwa mkusanyiko huo ulikuwa na nia ya kufanya uvunjifu wa amani na kusababisha Taharuki kwa wananchi.


Washtakiwa wote walikana shtaka hilo na wapo nje kwa dhamana kwa kila mshtakiwa kuwa na mdhamini mmoja ambaye alisaini ahadi ya Shilingi Milioni 1. 5 na wasitoke nje ya jiji la Dar es Salaam bila ya kuwa na kibali cha mahakama. Upelelezi bado haujakamilika. Kesi imeahirishwa hadi March 8,2018.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527