RUKWA WACHOMA MISITU KUTAFUTA PANYA KWA AJILI YA KITOWEO..MKAKATI KABAMBE WAANDALIWA


Serikali mkoani Rukwa imesema inafanya mkakati wa kuwamaliza panya wote porini kwani wamekuwa ni sababu ya wakazi wa mkoa huo kuchom amoto misitu kwa nia ya kutafuta panya ili watumie kama kitoweo

Akizungumza jana wakati wa kampeni ya upandaji miti kwa lengo la kuhifadhi mazingira katika Kijiji cha Mpwapwa, kata ya Mpwapwa, Wilayani Sumbwanga mkuu wa mkoa huo Joachim Wangabo alimuagiza mkuu wa wilaya ya Sumbawanga Dkt. Khalfan Haule ahakikishe anatafuta dawa ya kuua panya porini ili kuokoa miti kwani baadhi ya watu wamekuwa wakichoma moto misitu kwa ajili ya kuwindaji wa panya.

Alisema kuwa amesikia changamoto hiyo ya uchomaji wa misitu kwa sababu ya uwindaji wa panya kutoka kwa vijana mbalimbali wanaojishughulisha na mashamba ya upandaji miti pamoja na taarifa iliyosomwa na mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Sumbawanga juu ya changamoto za kuendeleza misitu.

“DCnakuagiza tafuta dawa ya panya, wauliwe huko mashambani na porini ili panya wasiwepo na miti iokoke, mbona hamshangilii? hawa panya tutawaua kwa sumu huko mashambani wasiwe chanzo cha moto ambao mnachoma huko kuwatafuta wafie huko huko mashimoni msiwapate,” alisema.

Pia alimuagiza mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya hiyo kuhakikisha anasimamia sheria ya hifadhi ya mazingira na kuwawajibisha wote wanaohusika na uharibifu wa mazingira ambapo mkuu huyo wa mkoa alitoa miche 850 kwa kaya 850 za kijiji cha Mpwapwa ili ipandwe kila kaya mti mmoja.

Awali akisoma taarifa mkurugenzi wa halmashauri hiyo John Msemakweli alibainisha kuwa miongoni mwa changamoto ni muitikio mdogo wa uhifadhi wa mazingira pamoja na mila na tamaduni za wananchi za uwindaji wa panya hali inayosababisha uchomaji wa misitu wakati wa kiangazi.

“Changamoto nyingine ni baadhi ya viongozi wa serikali ya kijiji kujihusisha na uuzajia wa maeneo yaliyotengwa kwaajili ya hifadhi ya Kijiji na usimamizi mdogo wa sheria ndogo za vijiji katika utunzaji wa misitu,”alisema.

Katika msimu wa mwaka 2017/2018 hadi 30/1/2018 halmashauri ya wilaya ya Sumbwanga imepanda miti 830,527 ambayo ni sawa na asilimia 55.4 na ina misitu 92 yenye ukubwa wa hekta 49,179.6. 

Mmoja wa wakazi wa kijiji hicho Steven Sichula alilipokea kwa masikitiko agizo hilo la mkuu wa mkoa kwani alisema kuwa sio haki kuwamaliza panya wote kwani nao ni viumbe hai wanahitaji kuishi na ni kitoweo kwao kwani wanapata protini ambapo alishauri utafutwe utaratibu mwingine wa kukomesha tabia hiyo lakini si kuwaua panya wote.
Na Walter Mguluchuma - Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527