RAIS MAGUFULI AMTEUA DKT OMARI RASHID NUNDU KUWA MWENYEKITI WA BODI YA TTCL

China imeridhia kutoa msaada wa Dola za Marekani Milioni 62 sawa na Shilingi Bilioni 138.3 za Tanzania kwa ajili ya ujenzi wa Chuo Kikuu cha Usafirishaji hapa nchini.


Balozi wa China hapa nchini Mhe. Wang Ke amesema hayo leo tarehe 12 Februari, 2018 muda mfupi baada ya kufanya mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt John Pombe Magufuli na kumkabidhi barua yenye ujumbe wa Rais wa China Mhe. Xi Jinping, Ikulu Jijini Dar es Salaam.


Mhe. Wang Ke ameeleza kuwa msaada huo ni sehemu ya misaada na miradi mbalimbali ambayo China inaitekeleza hapa nchini Tanzania yenye lengo la kuimarisha uhusiano na ushirikiano kati yake na Tanzania.


Kwa upande wake Mhe. Rais Magufuli amemuomba Mhe. Wang Ke kumfikishia shukrani zake kwa Rais wa China kwa ujumbe na msaada huo ambao amesema utasaidia kuimarisha huduma za usafirishaji hapa nchini.


Wakati huo huo, Mhe. Rais Magufuli amepokea taarifa kutoka kwa viongozi wa Shirika la Simu Tanzania kuhusu mwelekeo wa shirika hilo baada ya kuanza kutumika kwa sheria namba 12 ya mwaka 2017 ya Shirika la Simu Tanzania, iliyolibadili kutoka Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL) na kuwa Shirika la Simu Tanzania (TTCL Corporation) kuanzia tarehe 01 Februari, 2018.


Pamoja na kupokea taarifa hiyo Mhe. Rais Magufuli amemteua Dkt. Omari Rashid Nundu kuendelea kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya TTCL Corp na Bw. Waziri Waziri Kindamba kuwa Mkurugenzi Mkuu wa TTCL Corp, na amewataka kuchapa kazi kwa juhudi na kuhakikisha TTCL Corp inaongeza ufanisi, na kutoa gawio kwa Serikali.


Dkt. Omari Rashid Nundu na Bw. Waziri Waziri Kindamba wamemshukuru Mhe. Rais Magufuli kwa uteuzi huo na wamesema TTCL itaendelea kujiimarisha kwa kupanua huduma za mawasiliano nchini, kuongeza na kuboresha bidhaa ikiwemo TTCL Pesa, kuzalisha faida zaidi na kuusimamia vizuri mkongo wa Taifa kwa maslahi na usalama wa nchi.


Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es Salaam
12 Februari, 2018

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527