WATOTO 67 WAKATALIWA NA FAMILIA ZAO






Watoto 67 wilayani Tarime mkoani Mara wamekataliwa na familia zao baada ya kukataa kukeketwa na kukimbilia kwenye kituo cha kuhifadhi wasichana wanaokataa kutekeleza mila hiyo.


Watoto hao wametua na kupokewa na kituo cha Association For Termination of Female Genital Multilation (ATFGM Masanga) kilichopo mjini hapa. Kufuatia hatua hiyo, Serikali imewataka wazazi hao kutoa malezo ya kuwakataa watoto wao baada ya kukataa kufanyiwa unyama huo kabla hawajachukuliwa hatua za kisheria.


Akitoa agizo hilo kwa niaba ya mkuu wa Wilaya ya Tarime, Glorious Luoga, kaimu ofisa elimu msingi wa halmashauri ya Wilaya ya Tarime, Amos Waitara alivitaka vyombo husika vya Serikali kuhakikisha watoto hao wanapata haki za malezi kutoka kwa wazazi wao.


Waitara alitoa agizo hilo wakati wa kufunga kambi ya wasichana 103 waliokuwa wamekimbilia katika kituo hicho na kupewa mafunzo mbadala dhidi ya madhara ya ukeketaji na tohara.


“Hatuwezi kulifumbia macho suala hili kwa baadhi ya wazazi hawa kuminya uhuru wa watoto walioona mbali na kuchukua jukumu la kupinga vitendo vya kikatili vya ukeketaji, wazazi hao waitwe na kueleza kwa maandishi sababu za kuwanyanyasa,” alisema .


Meneja miradi ATFGM, Valerian Mgani alisema tangu kituo hicho kilipoanzishwa mwaka 2008 wamekuwa wakipokea watoto ambao wanakimbia ukeketaji.


Wasichana hao hutoka wilaya za Serengeti, Tarime, Loliondo na nchi jirani ya Kenya na kambi inapomalizika hurudishwa nyumbani na baadhi yao wamekuwa wakikataliwa na wazazi.


Naomi Baraka kutoka nchi jirani ya Kenya ambaye alishiriki mafunzo hayo ya tohara mbadala, aliiomba Serikali ya Kenya kuthamini watoto wa kike huku akiitaka jamii kuondokana na mila ambazo zimepitwa na wakati.


Baadhi ya mabinti ambao hawakutaka kutaja majina yao kutoka kata za Sirari, Pemba na Nyanungu wilayani Tarime waliolazimishwa kuolewa katika umri mdogo na kukimbilia kituoni hapo waliiomba Serikali kuingilia kati jambo hilo. Kituo cha ATFGM Masanga mpaka sasa kina mabinti 2,572.

Na Waitara Meng’anyi, Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527