BABU SEYA NA WANAE WAIBUKIA IKULU, RAIS MAGUFULI AWATAKA WAKACHAPE KAZI

Rais Dkt John Pombe Magufuli akiwa ameshikana Mikono na kuomba dua na Mwanamuziki Nguza Vicking “Babu Seya” na wanae Johnson Nguza “Papii Kocha”, Francis Nguza na Michael Nguza walipofika Ikulu jijini Dar es salaLeo Januari 2, 2018 kumshukuru kwa msamaha wake aliotoa kwao dhidi ya kifungo cha maisha walichokuwa wakitumikia.


Mwanamuziki Nguza Vicking “Babu Seya” na wanae Johnson Nguza “Papii Kocha”, Francis Nguza na Michael Nguza walipofika Ikulu jijini Dar es salaam leo Januari 2, 2018 kumshukuru Rais Magufuli kwa msamaha wake aliotoa kwao dhidi ya kifungo cha maisha walichokuwa wakitumikia gerezani tangu walipohukumiwa miaka 13 iliyopita.
***

Rais John Magufuli amekutana na mwanamuziki Nguza Viking na watoto wake waliofika Ikulu jijini Dar es Salaam kumshukuru kwa kuwapa msamaha uliowawezesha kutoka gerezani.


Nguza Viking ‘Babu Seya’ na mwanaye Johnson Nguza ‘Papii Kocha’ walikuwa wakitumikia kifungo cha maisha jela na waliachiwa kwa msamaha wa Rais alioutoa Desemba 9,2017 wakati wa maadhimisho ya miaka 56 ya Uhuru wa Tanganyika.


Nguza na mwanaye waliokuwa wakishikiliwa katika Gereza la Ukonga ni miongoni mwa wafungwa 8,157 wakiwemo wa vifungo vya maisha na waliohukumiwa kunyongwa hadi kufa waliopata msamaha wa Rais.


Wawili hao walikaa gerezani kwa takriban miaka 13 na miezi minne baada ya kutiwa hatiani na kuhukumiwa adhabu hiyo kwa kosa la kubaka na kulawiti watoto 10 waliokuwa wanafunzi wa Shule ya Msingi Mashujaa iliyopo Sinza, Dar es Salaam.


Taarifa iliyotolewa na Ikulu leo Jumanne Januari 2,2017 imesema Nguza na Johnson wakiwa na wanafamilia wengine Nguza Mbangu na Francis Nguza wamezungumza na Rais Magufuli wakimshukuru kwa msamaha huo.


Akina Nguza wamemuahidi Rais kwamba watakuwa raia wema na watachapa kazi kwa juhudi na maarifa.


Msemaji wa familia hiyo, Mbangu amesema wanajipanga kuendeleza kazi zao za sanaa. Pia walimuombea Rais Magufuli na Taifa.


Rais Magufuli amewashukuru kwa kwenda kumuona na kumshukuru, akisema shukrani zimwendee Mwenyezi Mungu ambaye ndiye husamehe.


"Najua mmekuwa mkihangaika kutaka kuniona nikaona wacha niwasikilize, hata hivyo mshukuruni Mwenyezi Mungu ambaye ndiye hutoa msamaha, sasa nendeni mkachape kazi na mumtangulize Mungu," amesema Rais Magufuli.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527