RAIS MUGABE AMEMFUTA KAZI MAKAMU WA RAIS

Emmerson Mnangagwa

Taarifa kutoka Harare zinasema kwamba, Makamu wa rais wa Zimbabwe, Emmerson Mnangagwa amefutwa kazi.

Bw. Mnangagwa mwenye umri wa miaka 75, ameachishwa kazi kwa madai kuwa alionyesha tabia za kukosa uzalendo na uaminifu hasa kwa Rais. 

Hayo yamesemwa na Waziri wa Habari wa Zimbabwe Simon Kahaya Moyo.

Kufutwa kwake ni ishara kuwa mke wa rais Robert Muabe, Bi Grace, atafuata nyayo za mumeme za kuwa rais wa Zimbabwe.

Siku ya Jumapili Bi Grace Mugabe alitoa wito wa kutaka mumewe amfute kazi Mnangagwa.

Bwana Mnangagwa, ambaye ni mkuu wa zamani wa idara ya ujasusi, amekuwa kwenye mstari wa mbele kumrithi Rais Mugabe.

Kufutwa kwake kunakuja baada ya Rais Robert Mugabe, 93, kutishia kumuachisha kazi Bw Mnangagwa, hatua ambayo imezua uvumi kuwa anataka mke wake kuchukua hatamu za kuliongoza taifa hilo.

Akihutubia mkutano wa wanachama wa makanisa ya asili mji Harare siku ya Jumapili, Bi Mugabe alisema:

"Nyoka ni lazima apiwe kwenye kichwa. Lazima tukabiliane na nyoka mwenyewe anayehusika na migawanyiko chamani. Tunaelekea kwenye mkutano tukiwa chama kimoja."

Bw Mugabe alimtaka Mnangagwa na wafuasi wake kumuonyesha uzalendo au afutwe kazi.

Chama cha Zanu-PF kinatarajiwa kuifanyia mabadiliko katiba yake wakati wa mkutano na kuweka nafasi mbili za makamu wa rais, nafasi moja ikiwa ni ya mwanamke.

Nafasi hiyo inatarajiwa kujazwa na Bi Mugabe na kuongeza uwezekano wa kumrithi mume wake.

Chanzo-BBC

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527