KANISA KATOLIKI LAKATAA KUMZIKA BILIONEA FAUSTINE MREMA


Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Arusha, limekataa kuendesha misa ya maziko ya mfanyabiashara bilionea Faustine Mrema kwa madai hakuwa na Sakramenti ya ndoa na mke wake wala kipaimara.

Paroko Msaidizi wa Parokia ya Mtakatifu Theresia, Mtoto Yesu, Jimbo Kuu la Arusha Padri Festus Mangwangi amekiri suala hilo na kuongeza kuwa marehemu enzi za uhai wake hakuweka heshima na kanisa.

“Marehemu ni mkatoliki wa kuzaliwa, lakini hakuwahi kuwa na sakramenti ya ndoa na mke aliyezaa naye watoto wala kupata Kipaimara. Kanisa haliwezi kumzika kabisa, kawaida mazishi ya Kanisa Katoliki ni heshima inayotolewa kwa mhusika kama anastahili.

“Huyu hakuwahi kufunga ndoa kanisani, alijitenga na kanisa kwa hiyo kusema tumemtenga si kweli, yeye ndiyo alijikataa hakutaka kutafuta heshima yake na kanisa akiwa hai,” alisema Padri Mangwangi.

Kuhusu kutokwenda kwenye Misa za Jumuiya ambayo nayo ni moja ya taratibu muhimu inayowataka waumini wa kikatoliki kushiriki ibada za nyumba kwa nyumba Padri Mangwangi amesema, hata ibada hizo nazo pia marehemu alikuwa hashiriki.

“Jumuiya ni utaratibu wa kanisa unaowataka waumini wawe na ushirika wa karibu ikiwamo kufahamiana marehemu pia alikuwa hashiriki kabisa sasa unaanzaje kumzika mtu kwa heshima za Kanisa Katoliki?” amehoji Padri Mangwangi.

Wakati Kanisa hilo likijivua kushiriki Misa ya heshima ya maziko ya marehemu Mrema hiyo jana, Askofu Dk. Eliud Issangya wa Kanisa la Kimataifa la Kiinjili, alilazimika kuongoza Ibada hiyo ya maziko iliyofanyika Hoteli ya Ngurdoto, wilayani Arumeru.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post